Hofu mizozo ya kikabila ikizuka Tana River uchaguzi ukikaribia
HOFU ya mapigano ya kikabila imeibuka tena katika Kaunti ya Tana River baada ya matukio mawili yaliyotokea ndani ya wiki mbili, kuzua wasiwasi kuhusu kuongezeka kwa mivutano ya kijamii.
Tukio la hivi punde lilitokea Jumamosi, Juni 20, wakati mamia ya wakazi walipovamia Kituo cha Polisi cha Bangale na kumtorosha kiongozi wa vijana aliyekuwa amekamatwa kwa madai ya kuhamasisha mashambulizi dhidi ya wanajamii wa kabila jingine.
Kwa mujibu wa ripoti ya polisi, maafisa wakiongozwa na Mkuu wa Upelelezi wa Uhalifu wa Kaunti Ndogo ya Bangale, Bw Michael Lemaiyan, walimkamata mshukiwa anayedaiwa kuwa kiongozi wa vijana wa jamii ya Wardey.
Mshukiwa huyo alidaiwa kuhusika katika kuwachochea wanajamii wake dhidi ya jamii ya Degodia.
Polisi walisema walipata Sh340,000 nyumbani kwake, fedha wanazoamini ni sehemu ya Sh1 milioni zinazodaiwa zilikusudiwa kutumika katika shughuli za uchochezi.
Baada ya kushughulikiwa katika Kituo cha Polisi cha Bangale, mshukiwa huyo alikuwa akisafirishwa kwenda Kituo cha Polisi cha Madogo wakati umati wenye hasira wa karibu watu 300 ulipovamia kituo hicho, kuzuia lango na kuanza kuwarushia mawe maafisa wa polisi.
Polisi walirusha vitoa machozi na kufyatua risasi hewani kujaribu kuwatawanya watu hao, lakini umati huo uliwashinda nguvu na kufanikiwa kumtorosha mshukiwa.
“Magari mawili, yaliharibiwa baada ya vioo vya mbele kuvunjwa. Hakuna aliyeripotiwa kujeruhiwa,” polisi walisema.
Baadaye, kikosi cha Rapid Deployment Unit kutoka Katumba kilifika na kufanikiwa kuwatawanya watu hao.
Kundi hilo pia lilijaribu kuzuia barabara kuu ya Mwingi-Garissa lakini lilizuiwa na maafisa wa usalama.
Polisi walisema maafisa wamekuwa wakishika doria katika kituo cha biashara cha Bangale ili kuzuia mashambulizi dhidi ya nyumba na biashara zinazomilikiwa na wanajamii wa Degodia.
Mamlaka zilisema hali imeendelea kuwa shwari.
Tukio hilo lilijiri chini ya wiki mbili baada ya makabiliano mengine kati ya polisi na watu wenye silaha katika eneo la Biyagadud.
Maafisa waliokuwa wakijibu tukio la ufyatuaji risasi lililotokea mapema Juni 7, walikumbana na karibu watu 40 wenye silaha wanaodhaniwa kutoka jamii ya Wardey.
Polisi walisema kundi hilo, ambalo lilikuwa limepeleka mbuzi katika eneo hilo, lilianza kuwafyatulia risasi maafisa wa polisi, hali iliyosababisha mapambano.
Maafisa kutoka Kituo cha Polisi cha Bangale walijibu mashambulizi hayo na kuondoka eneo hilo bila kujeruhiwa.
Kamanda wa Polisi wa Ukanda wa Pwani, Bw Ali Nuno, alisema maafisa wa kutosha washapelekwa eneo hilo kudhibiti hali.
“Hii ni operesheni ya pamoja ya vyombo mbalimbali vya usalama na tutahakikisha kuwa mambo yanakuwa shwari,” alisema Bw Nuno.
Polisi wanashuku kuwa watu hao wenye silaha walifyatua risasi kwa lengo la kuwatisha wakazi na kupata nafasi ya maji na malisho kwa mifugo yao.
Mivutano hiyo imezua hofu ya kurejea kwa mapigano ya kikabila Tana River, huku baadhi ya wanasiasa wa eneo hilo wakihusisha machafuko hayo na maandalizi ya kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027 katika eneo ambalo siasa za kikabila bado zina ushawishi mkubwa.