Habari

Vita vya ubabe vyatatiza shughuli idara ya polisi

Na KAMORE MAINA June 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MGOGORO wa muda mrefu wa kupigania mamlaka kati ya makamishna raia wa Tume ya Kitaifa ya Huduma ya Polisi (NPSC) na wakuu wa polisi umelemaza oparesheni zinazohusu waajiriwa.

Mzozo huo umeathiri kupandishwa vyeo kwa maafisa wa polisi, hali ambayo imeripotiwa kudidimiza motisha ya maafisa katika Huduma ya Polisi nchini (NPS).

Kwa sababu ya vita vya kupimana ubabe vinavyohusisha tume inayoongozwa na mwenyekiti Dkt Yuda Komora dhidi ya makamanda wakiongozwa na Inspekta Jenerali wa Polisi, Douglas Kanja, tume hiyo inayowajibikia usimamizi wa wafanyakazi katika NPS, wanaojumuisha Huduma ya Polisi Kenya, Polisi wa Utawala na Idara ya Uchunguzi kuhusu Uhalifu, haijakutana tangu Oktoba mwaka uliopita.

Uhasama huo uliotokota kwa muda mrefu ulishika kasi kufuatia usajili uliopingwa vikali wa maafisa 10,000 mwaka uliopita ambapo wakuu wa polisi walipuuzilia mbali mwongozo wa tume.

Walidai kuwepo njama za kutwaa mamlaka ya Inspekta Jenerali na kusababisha kesi kortini ambapo amri ilitolewa Februari kusimamisha michakato yote ya upandishaji vyeo na kufuta kazi hadi itakaposikizwa na uamuzi kutolewa.

Ukosefu wa tume inayofanya kazi umeelekea kulemaza oparesheni za polisi.

Duru zilisema kuwa maafisa waliohudhuria kozi za kupandishwa vyeo wangali wamekwama kwenye nyadhifa zao za zamani kwa sababu ni sharti tume ipitishe nyadhifa mpya.

Tume ina jukumu la kuthibitisha maafisa kutoka daraja ya afisa msimamizi baada ya kuhudhuria kozi za kupandishwa cheo.

Maafisa wanaohamishwa katika afisi mpya vilevile wanashindwa kutekeleza wajibu wao ipasavyo kwa sababu baadhi yao bado hawajapata hadhi mpya zinazoambatana na afisi mpya.

Kwa mfano, katika makao makuu ya Kitengo cha Polisi wa Kuzima Fujo, kamanda mpya wa GSU, Johana Tonui bado hajathibitishwa kujiunga na daraja mpya kufuatia uteuzi wake.

Bw Tonui, naibu inspekta jenerali, anachukua usukani kutoka kwa Bw Ranso Lolmodooni, ambaye amestaafu.

Anahitajika kupandishwa cheo kutwaa wadhifa mpya wa Naibu Mkuu wa Inspekta Jenerali wa Polisi SAIG) kusimamia GSU.

Matokeo ni kwamba, duru zinasema kulemazwa huko kumezua malalamishi ndani ya kikosi cha polisi na kuvutia mamlaka katika ngazi za juu, kukiwa na wasiwasi kwamba huenda ikaathiri maandalizi ya kiusalama kabla ya uchaguzi mkuu Agosti mwaka ujao.

Naibu Rais Prof Kithure Kindiki Alhamisi iliyopita aliitisha kikao katika makazi yake rasmi Karen kati ya makundi yanayozozana kujaribu kuyapatanisha.

Miongoni mwa masuala ambayo hayajasuluhishwa ni mvutano kati ya makundi mawili hayo kuhusu udhibiti wa Sh60 bilioni za mishahara ya polisi.

Ikiwa tume huru iliyobuniwa chini ya Katiba 2010, NPSC ilichukua usukani, miongoni mwa majukumu mengine, wajibu wa kusimamia waajiriwa wa huduma ya polisi ambao mbeleni ulishughulikiwa na Tume ya Kuajiri Watumishi wa Umma.