Macho sasa yaelekezwa kwa Gavana Mutula Kilonzo kuhusu sakata ya maembe Makueni
DARUBINI sasa imeelekezwa kwa Gavana wa Kaunti ya Makueni, Mutula Kilonzo Junior, baada ya madiwani kuwalaumu maafisa wa kaunti kwa kuhusika katika sakata ya maembe ya Sh20 milioni iliyoacha maelfu ya wakulima wakihesabu hasara.
Mnamo Jumanne, madiwani wa kaunti ya Makueni walipitisha ripoti ya kamati ya pamoja ya Hesabu za Umma na Uwekezaji wa Umma iliyoongozwa na MCA wa Masongaleni, Bw Bryan Nzoka.
Spika wa Bunge la Kaunti, Bw Douglas Mbilu, alisema ripoti hiyo itawasilishwa kwa gavana, naibu wake, Waziri wa Kilimo, pamoja na bodi ya Mamlaka ya Ukuzaji na Uuuzaji wa Matunda ya Kaunti ya Makueni kwa utekelezaji wa haraka.
Ripoti hiyo inaeleza jinsi Kiwanda cha kuchakata matunda cha Makueni, kilichokusudiwa kupunguza hasara baada ya mavuno, kilivyoshirikiana na baadhi ya maafisa wa kaunti na viongozi wa vyama vya ushirika kukwepa taratibu za uadilifu katika ununuzi wa maembe.
Kulingana na makubaliano, kila chama cha ushirika kati ya saba kilitakiwa kuwasilisha tani 10 za maembe kwa siku.
Hata hivyo, siku ya kwanza, vyama vya Kika Farmers, Mulili Kyale na Makuwo Farmers viliwasilisha tani 42, 72 na 73 mtawalia, hali iliyozua tuhuma kuwa baadhi ya maembe yaliingizwa kutoka Tanzania.
Kamati ilipendekeza hatua za kinidhamu, ikiwemo kufutwa kazi kwa Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo, Bw Joseph Kioko, kwa kuruhusu maembe ya ziada na matumizi yasiyoidhinishwa ya gari la serikali kusafirisha mazao bila stakabadhi halali.
Pia ilimtaka Waziri wa Kilimo wa kaunti kuanzisha hatua dhidi ya maafisa wa kilimo na maafisa wengine waliotajwa kughushi stakabadhi za ununuzi.
Hata hivyo, kamati haikuwachunguza baadhi ya madiwani na maafisa wakuu waliotajwa kuhusika, ikitaja ukosefu wa muda.
Hatua hiyo imeibua maswali mapya, huku baadhi ya madiwani wakidai ripoti haikubainisha chanzo cha maembe yote yaliyowasilishwa kiwandani.
Wakulima wadogo walioathirika wameendelea kushinikiza walipwe fidia wakisema maembe yao yaliharibika kutokana na sakata hiyo.
Aidha, chama cha wafanyakazi wa serikali za kaunti kimejitokeza kuwatetea maafisa waliotajwa, kikidai wanatolewa kafara kisiasa.
Sasa macho yote yako kwa utawala wa gavana kuona iwapo mapendekezo hayo yatatekelezwa na wakulima kupata haki yao.