Habari

Mmiliki wa duka la kubadilishana pesa za kigeni ashtakiwa kwa ulaghai wa dhahabu

Na RICHARD MUNGUTI February 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MMILIKI wa duka la kubadilisha pesa za kigeni ameshtakiwa kwa ulaghai wa USD250,500 (KSh32.3 milioni) katika kashfa ya dhahabu.

Mohammed Noor alishtakiwa katika mahakama ya Milimani Nairobi kwa kula njama za kumlaghai wakili John Sodipo wa kampuni ya mawakili ya Sodipo Group USD250,500 (KSh32,314,500).

Akipokea pesa hizo mahakama ilielezwa Bw Noor alidai alikuwa na uwezo wa kuyeyusha kilo 495 za dhahabu na kuzisafirisha kwa Meli kutoka Kenya hadi Dubai.

Hakimu mkazi mahakama ya Milimani Irene Kamara alielezwa Bw Noor ambaye pia amebobea katika uuzaji wa simu za rununu katika eneo la Luthuli Avenue Nairobi alishtakiwa kuhifadhi pesa zilizopatikana kwa njia ya ulaghai.

Mahakama ilielezwa mshtakiwa aliweka pesa hizo katika akaunti ya Mohazoom Trading katika benki ya National Bank NBK.

Bw Noor pia alikabiliwa na shtaka la kutumia kitita cha USD217,900 (KSh28,109,100) akijua zimepatikana kwa njia ya ulaghai.

Alikana shtaka na kuachiliwa kwa dhamana ya Sh350,000 pesa tasilimu.

Kesi hiyo itatajwa Machi 2, 2026 ili Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma aiunganishe na nyingine.