Maafisa watibua shambulio kubwa la kigaidi kipindi cha Ramadhani
MAAFISA wa usalama nchini wamefanikiwa kutibua hatari wanayoitaja kama shambulio kubwa la kigaidi lililopangwa kutekelezwa jijini Nairobi wakati wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, kwa kuvuruga mtandao unaochukuliwa kuwa na uhusiano na kundi la kigaidi la Al-Shabaab lenye makao yake nchini Somalia.
Operesheni hiyo iliyotekelezwa usiku wa Jumanne ilikuwa kilele cha wiki kadhaa, na huenda miezi, ya kazi ya kijasusi iliyoongozwa na maafisa wa Huduma ya Kitaifa ya Ujasusi (NIS) wakishirikiana na Kikosi Maalum cha Operesheni (SOG), kinachojumuisha maafisa kutoka idara mbalimbali za usalama.
Kwa mujibu wa vyanzo vya ndani ya idara za usalama, washukiwa 13 walikamatwa wakiwa njiani kuelekea Nairobi. Kundi hilo linajumuisha Wakenya 10, Watanzania wawili na raia mmoja wa Uganda.
Inadaiwa walikuwa katika hatua za mwisho za kukamilisha mipango ya shambulio lililoratibiwa kulenga maeneo yenye idadi kubwa ya watu wakati wa Ramadhani.
Kambi ya wakimbizi ya Daadab imetajwa kama moja ya vituo vilivyotumiwa na washukiwa hao kuratibu shughuli zao.
Maafisa wanasema baadhi ya washukiwa walikuwa wakifanya kazi kama mawakala wa kupokea na kuhamisha fedha zinazodhaniwa kufadhili shughuli za itikadi kali katika ukanda wa Afrika Mashariki.
“Walitambuliwa pia kama mawakala wa kupokea na kuhamisha fedha kusaidia shughuli za kigaidi katika eneo hili. Nairobi iko salama kutokana na juhudi za idara zetu za usalama. Maafisa wetu wanaendelea kufuatilia wote wanaohusishwa na mitandao hii hatari,” Kitengo cha Kupambana na Ugaidi kilisema katika taarifa rasmi.
Wakati wa operesheni hiyo, maafisa walinasa silaha na vifaa mbalimbali, kilomita chache kutoka jijini.
Miongoni mwa silaha zilizonaswa ni bunduki tano aina ya AK-47, risasi 600 – kiasi kinachoweza kuendeleza mapigano kwa muda mrefu gruneti sita na bastola moja aina ya Makarov yenye risasi 24 za milimita tisa.
Mbali na silaha hizo, kulipatikana pia vifaa vya matibabu, zikiwemo bandeji za kufunga majeraha, sindano za kusaidia damu kuganda, dawa za kupunguza maumivu aina ya diclofenac, paracetamol (Tekomol), dawa ya kupunguza asidi tumboni, sindano nne za matumizi ya mara moja pamoja na katoni mbili za tende, chakula chenye nishati ya haraka.
Kwa mujibu wa wachunguzi, uwepo wa vifaa hivyo unaonyesha kuwa kundi hilo lilikuwa limejiandaa si kwa shambulio la ghafla tu bali pia kuendeleza operesheni kwa muda mrefu endapo lingefanikiwa kutekeleza mpango wake.
Vifaa vya matibabu vinaashiria maandalizi ya kukabiliana na majeraha vitani, huku chakula kikionyesha mipango ya kustahimili mazingira katika maficho.
Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi, Bw Gilbert Masengeli, alisema operesheni hiyo ilitekelezwa kwa msingi wa habari za kina za ujasusi zilizokusanywa kwa muda.
“Hii ilikuwa operesheni iliyoongozwa na taarifa za kijasusi kwa ushirikiano na SOG. Tulifanikiwa kuzima mpango wao katika hatua za awali kabla haujatekelezwa. Uchunguzi wa awali unaonyesha walinuia kulenga maeneo yenye watu wengi wakati wa Ramadhani. Tunawasihi wananchi wawe macho na watoe taarifa kuhusu chochote kinachotia shaka,” alisema.
Chanzo cha ngazi ya juu katika Ofisi ya Rais kilidokeza kuwa operesheni hiyo imezuia maafa makubwa ambayo yangeathiri mamia ya wananchi wasio na hatia.
Hata hivyo, hakikutoa maelezo ya kina kuhusu waliokusudiwa au maeneo mahsusi yaliyokuwa yanalengwa, kikisema uchunguzi bado unaendelea ili kuvunja mtandao mzima na ufadhili.
Maafisa wa usalama walisema mawasiliano yaliyodukuliwa katika siku za karibuni yalionyesha nia ya kutekeleza mashambulizi na hata uwezekano wa utekaji nyara, mbinu ambayo makundi ya kigaidi hutumia kuvuta umakini wa kimataifa na kupata fedha kupitia fidia.
Katika miaka ya hivi karibuni, Kenya imebadilisha mkakati wake wa kupambana na ugaidi kwa kuelekeza nguvu zaidi katika kuzuia mashambulizi kabla hayajatokea badala ya kusubiri na kujibu baada ya tukio.
Mabadiliko haya yalichochewa na uzoefu wa mashambulizi ya awali yaliyotikisa taifa, yakiwemo ya Westgate mwaka 2013, Chuo Kikuu cha Garissa mwaka 2015 na jengo la DusitD2 mwaka 2019.
Wachambuzi wa masuala ya usalama wanasema makundi yenye misimamo mikali yamebadili mbinu, yakiepuka mashambulizi makubwa yanayovutia macho na badala yake kuunda makundi mandogo ambayo ni vigumu kugundua.
Operesheni ya Jumanne inaonyesha kuwa idara za usalama pia zimeboresha mbinu zao za kukabiliana na changamoto hizo.
Kwa sasa, wachunguzi wanachambua vifaa vya kielektroniki, stakabadhi na rekodi za kifedha zilizonaswa ili kufuatilia njia za ufadhili, mbinu za uajiri na uwezekano wa kuwepo kwa wahusika kutoka nje ya nchi.
Inatarajiwa kuwa maafisa wataomba mahakama iwaruhusu kuwazuilia washukiwa kwa muda mrefu zaidi uchunguzi ukipanuliwa.