Siasa

Rekodi yako pekee mamlakani ni kuuza ardhi ya shule Ruaraka, Kindiki amsuta Matiang’i

Na JUSTUS OCHIENG February 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAJIBIZANO makali ya kisiasa yamezuka kati ya Naibu Rais Kithure Kindiki na aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i kuhusu sakata tata ya ardhi ya Ruaraka, huku wawili hao wakirushiana lawama kali zinazoashiria mapambano ya mapema kuelekea uchaguzi wa urais wa 2027.

Kilichoanza kama ukosoaji mkali katika kongamano la wagombea wa United Democratic Alliance (UDA) lililofanyika Ikulu, Nairobi, sasa kimegeuka kuwa pambano kuhusu uwajibikaji, uongozi na urithi wa utawala uliopita.

Akizungumza Februari 4, Profesa Kindiki alimshutumu Dkt Matiang’i, anayewania urais kupitia tiketi ya Jubilee Party, kuwa sehemu ya serikali iliyoacha changamoto sugu katika sekta muhimu, hasa elimu.

Katika hotuba iliyoshangiliwa na wafuasi wa chama, Naibu Rais alipuuza ukosoaji wa Dkt Matiang’i dhidi ya utawala wa Kenya Kwanza, akiutaja kama unafiki.

“Nataka kuwaambia wanaozungumzia elimu, tunajaribu kurekebisha hali mliyoacha katika sekta ya elimu. Tutaweka bango likisema, ‘Kazi inaendelea. Msitusumbue; tunarekebisha matatizo mliyoacha katika sekta ya elimu,’” alisema Profesa Kindiki.

Kulingana naye, matatizo mengi yanayoikumba sekta ya elimu kwa sasa, ikiwemo changamoto za Mtaala wa Umilisi (CBC), uhaba wa walimu na madarasa, yalianza wakati Dkt Matiang’i alikuwa Waziri wa Elimu chini ya Rais (mstaafu) Uhuru Kenyatta.

Rais William Ruto alikuwa Naibu Rais katika utawala huo.

Hata hivyo, ni tamko la Profesa Kindiki kuhusu sakata ya ardhi ya Ruaraka yaliyopokewa kwa nderemo nyingi zaidi.

“Rekodi yao pekee walipokuwa mamlakani ni kuuza ardhi ya shule Ruaraka. Tunajua aliyeuza ardhi; watuache tufanye kazi. Tutawaaibisha,” alitangaza, kauli iliyotafsiriwa kama onyo la moja kwa moja kwa Dkt Matiang’i.

Sakata hiyo inahusu kipande cha ardhi kinachobishaniwa ambacho imejengwa shule za umma—Drive-In Primary School na Ruaraka High School.

Wakati wa uongozi wa Profesa Matiang’i katika Wizara ya Elimu, serikali ililipa Sh1.5 bilioni kama fidia kwa wawekezaji binafsi waliodai kumiliki ardhi hiyo, jambo lililozua ghadhabu ya umma.