Waumini wa Kiislamu wahimizwa kujiepusha na hasira, ugomvi
MAIMAMU na wahubiri wa Kiislamu Lamu na Pwani wamewahimiza waumini kujiepusha na hasira na ugomvi kipindi cha mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan kikianza.
Ramadhan ilianza rasmi juma hili ambapo waumini wa dini ya Kiislamu watajinyima kula, kunywa mchana kutwa kwa muda wa siku 30.
Wakizungumza na Taifa Leo, viongozi hao wa kiislamu walisema mara nyingi waumini wanaoshiriki saumu hujipata wakifeli kudhibiti hisia na ghadhabu, hivyo kuishia kugombana na wengine.
Imamu Mahmoud Ahmed, anasema ni wakati huu wa Ramadhan ambapo utapata baadhi ya ndoa zikivunjika kutokana na wanandoa kukosa kuvumiliana, hivyo kuishia kwenye mizozo au misukosuko ya kila mara.
Bw Ahmed aliwataka Waislamu kutambua kuwa hasira wakati wa Ramadhani ni jambo ambalo mara nyingi husababishwa na njaa, upungufu wa maji mwilini, na kushuka kwa kiwango cha sukari mwilini.
“Waumini wote walioko saumuni watambue kufunga kunapaswa kuwa na uvumilivu na utulivu. Huu ni wakati ambapo miili yetu itakuwa na upungufu wa maji, njaa na sukari kushuka damuni. Hapo ndipo utapata watu wakikosa kujizuia wanapokasirika. Ushauri wangu ni wao kujikaza na kustahimiliana. Msiwe wagomvi,” akasema Bw Ahmed.
Imamu wa Tudor, kaunti ya Mombasa, Bw Sharif Tantawy alisema kwa muumini wa dini ya Kiislamu anayeshiriki Ramadhan, kufunga sio kujizuia na chakula tu bali pia ni kulea nafsi.
“Tujitahidi kujizuia na hasira ili isipunguze thawabu za saumu zetu. Mizozo, ugomvi na hasira ni masuala yanayokinzana kabisa na lengo la uchamungu. Mtume wetu Muhammad (SAW) anatusisitizia kuwa mwenye nguvu ni yule anayejizuia wakati wa ghadhabu,” akasema Bw Tantawy.
Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Waislamu (SUPKEM), tawi la Lamu, Bw Mohamed Abdulkadir aliwashauri waumini kuzingatia hulka ya kusamehe, akiitaja kuwa sifa muhimu ya wachamungu.
Alishikilia kuwa Ramadhan, ni vyema watu kuwasamehe waliowakosea, akisema Mwenyezi Mungu anawapenda wafanyao wema na wanaodhibiti hisia zao, kama inavyoelezwa katika hadithi za Mtume.
“Tusamehe watu ili kupata radhi za Mwenyezi Mungu na kuingia peponi. Hiyo ni sehemu ya maandalizi ya wachamungu. Tujiepushe na hasira. Ni sehemu muhimu ya kukamilisha ibada ya saumu na kupata thawabu kamili,” akasema Bw Abdulkadir.