Makala

Trump aahidi Sh 908B kusaidia katika kuujenga upya Gaza

Na REUTERS, WINNIE ONYANDO February 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

RAIS wa Amerika, Donald Trump amezindua mkutano wa kwanza wa “Bodi yake ya Amani” mbele ya wawakilishi na waangalizi kutoka nchi 40.

Trump amesema kuwa Sh908 bilioni zimeahidiwa na wanachama tisa wa bodi hiyo kuwasaidia waathiriwa wa vita Gaza.

Ni asilimia 10 tu ya 908 bilioni zinazohitajika kuijenga upya Gaza baada ya uharibifu uliofanywa kutokana na vita vya miaka miwili kati ya Israeli na wanamgambo wa Hamas.

Rais huyo wa pia aliahidi Sh1.2 trilioni ila hakusema zitatumikaje.

Trump amesema kuwa Azerbaijan, Umoja wa Falme za Kiarabu, Morocco, Bahrain, Qatar, Saudi Arabia, Uzbekistan na Kuwait ndizo nchi zitakazochangia kitita hicho cha fedha za ujenzi wa Gaza.

“Ila la muhimu zaidi ni kuwa Bodi ya Amani itaongoza katika mpango wa kuijenga upya Gaza. Tutaifanya Gaza iwe mfano wa ufanisi, usalama na umoja. Na ni fahari kuwa mko hapa,” alisema Trump.

Mbali na ahadi za ufadhili, baadhi ya nchi zimesema zitatuma vikosi Gaza kama sehemu ya kikosi cha amani.

Nchi hizo ni Indonesia, Morocco, Kazakhstan, Kosovo na Albania.

Mkutano huo umefanyika huku kundi la waandamanaji kati ya 30 na 50 wakiwa wamekusanyika nje ya jengo ambalo mkutano huo ulikuwa ukifanyika.

“Bodi hiyo ya Amani” ya Trump ilitokana na mkataba wa amani uliopatikana kati ya Israeli na wanamgambo wa Hamas ili kuvimaliza vita vilivyokuwa vimedumu kwa miaka miwili.

Makubaliano hayo hayajavimaliza kabisa vita hivyo huku ripoti zikiarifu kuwa zaidi ya Wapalestina 600 wameuwawa tangu mkataba huo wa kusitisha mapigano ulipofikiwa.

Kumekuwa na ukosoaji kwamba Trump anajaribu kuuzima umuhimu wa Umoja wa Mataifa katika bodi yake hiyo.

Ifahamike kwamba Trump ameondoa pakubwa ufadhili wa Amerika katika Umoja wa Mataifa.