Upanuzi wa Bomas unaogharimu Sh41.9B waibua wasiwasi
MKAGUZI wa Hesabu za Serikali, Nancy Gathungu amefichua dosari kubwa katika mradi wa ukarabati wa Bomas of Kenya kwa thamani ya Sh41.9 bilioni, akisema mchakato huo ulikiuka sheria na haukufuata taratibu za ununuzi wa umma.
Kwa mujibu wa ripoti ya ukaguzi iliyowasilishwa Bungeni kupitia hesabu zilizokaguliwa za Wizara ya Ulinzi, Katibu wa wizara hiyo, Dkt Patrick Mariru, aliidhinisha ombi la ununuzi wa moja kwa moja mnamo Februari 17, 2025 ilhali hatua za zabuni zilikuwa tayari zimeanza, kama inavyothibitishwa katika hati za kutangaza zabuni na vyeti vya ukaguzi za eneo la mradi vya Februari 13 na 14, 2025.
Hatua hiyo ilikiuka Sheria ya Ununuzi wa Umma ya 2015.
Bi Gathungu pia aligundua kuwa mradi huo haukuwa katika bajeti mwaka wa kifedha 2024/25 kinyume cha Sheria ya Usimamizi wa Fedha za Umma (PFM) inayokataza matumizi au mikataba bila idhini ya Bunge la Kitaifa.
Mradi huo unalenga kubadilisha Bomas kuwa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (BICC) chenye uwezo wa kuketi hadi watu 11,000.
Hata hivyo, ripoti inaonyesha kuwa hadi Juni 30, 2025, Wizara ya Ulinzi ilikuwa imepokea Sh1.73 bilioni kutoka Idara ya Utamaduni, ambapo Sh1.5 bilioni zililipwa kama sehemu ya malipo ya awali ya asilimia 10 ya kandarasi ya thamani ya Sh4.2 bilioni.
Aidha, kulikuwa na mkanganyiko katika mpango wa ulipaji, ambapo mkataba ulitaja malipo kwa awamu tisa ndani ya miezi 24, ilhali Wizara ya Fedha iliidhinisha mpango wa malipo wa miaka 10. Kufikia Julai 2, 2025, mradi ulikuwa umefikia asilimia 12.9 ya utekelezaji huku malipo yakiwa asilimia 3.46 pekee.
Kwa mujibu wa sheria ya PFM, maafisa wahasibu wanaoidhinisha matumizi yasiyoidhinishwa wanaweza kuwajibishwa binafsi kwa hasara yoyote itakayopatikana.