Papa Leo XIV kuzuru Afrika kwa siku 10 Aprili
VATICAN CITY
KIONGOZI wa Kanisa Katoliki duniani Papa Leo XIV anatarajiwa kuzuru mataifa manne Afrika kati ya Aprili 13-23.
Vatican kupitia mawasiliano ilitangaza ziara hiyo ambapo Papa Leo atazitembelea Algeria, Angola, Equitorial Guinea na Cameroon.
Kabla ya hapo pia atakuwa na ziara ya siku moja Monaco mnamo Machi 28 kisha baada ya safari ya Afrika, atatua Uhispania kutoka Juni 6-12.
Wakati wa ziara yake Afrika, Papa Leo anatarajiwa kuvutia umati mkubwa na kuwashauri viongozi wa Afrika jinsi ya kuendeleza ziara hii.
Pia anatarajiwa kuzungumzia jinsi ya kuimarishwa kwa uhusiano kati ya Waislamu na Wakatoliki.
Tangu amrithi marehemu Papa Francis kuongoza kanisa Katoliki lenye zaidi ya wanachama bilioni 1.4 ulimwenguni, Papa amekuwa na ziara mbili pekee nje ya Vatican.
Alitembelea Uturuki na Lebanon mnamo Novemba na Desemba, japo ziara hizo awali zilistahili kufanywa na mtangulizi wake Papa Francis.
Mara ya mwisho Papa kutembelea Afrika, ilikuwa 2023 wakati ambapo Papa Francis alitembelea Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Sudan Kusini.
Papa Leo atakuwa papa wa kwanza kutembelea Algeria ambayo ni nchi ya Kiislamu japo pia ni sehemu ya historia ya kanisa Katoliki.