Habari za Kaunti

Himizo madereva watumie barabara ya Dongo Kundu badala ya feri

Na WINNIE ATIENO March 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAMLAKA ya bandari nchini (KPA) ambayo inasimamia huduma za feri, imewashauri madereva kutumia daraja la Dongo Kundu badala ya kivukio cha Likoni ili kupunguza msongamano.

Kupitia kwa taarifa, KPA imewarai madereva wanaovuka kutoka kisiwa cha Mombasa hadi ng’ambo ya pili ya Likoni wawe wakitumia barabara ya Dongo Kundu.

Madereva wengi wamekuwa wakipuuza daraja hilo ambalo lilijengwa kwa gharama ya Sh40 bilioni kuunganisha kaunti za Mombasa na Kwale na badala yake kusongamana katika kivukio cha feri ya Likoni.

Msongamano mkubwa hushuhudiwa wakati baadhi ya feri zinapokosa kuhudumu, kama vile jana ambapo feri tatu pekee kati ya tano zilikuwa kazini.

Mkuu wa mawasiliano wa KPA, Bw Sylvan Mghanga, alisema Wakenya wengi hawajui kuhusu daraja la Dongo Kundu na hivyo basi kung’ang’ania kuvuka katika kivukio cha Likoni hali inayosababisha msongamano mara kwa mara.

Aliwasihi madereva kutumia daraja hilo ambalo limerahisisha usafiri kutoka Kwale na Mombasa. Zaidi ya watu 300,000 hutumia kivukio hicho na magari 6,000 kwa siku.