Dimba

Hii imeenda? Arsenal yaimarisha udhibiti wa EPL Man City ikidondosha alama

Na MASHIRIKA March 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ARSENAL ilichukua udhibiti wa Ligi Kuu Uiongereza (EPL) wakishinda Brighton 1-0 ugenini huku Manchester City wakidondosha alama baada ya kutoka sare ya 2-2 nyumbani dhidi ya Nottingham Forest Jumatano usiku.

Vijana wa Mikel Arteta walienda katika mchuano huo wakihitaji ushindi wa lazima kwa sababu Manchester City walikuwa wakisoma mgongo wao.

Hata hivyo, Arsenal sasa itajilaumu iwapo itakosa kushinda ubingwa wa kwanza wa EPL tangu 2004 baada ya kufungua mwanya wa alama saba kileleni zikiwa zimesalia mechi nane msimu huu uishe.

Shuti ya Saka ilijazwa wavuni dakika ya sita huku Arsenal ikimaliza mechi ya 14 bila kufungwa msimu huu.

City nao watajilaumu wenyewe baada ya kuongoza mara mbili kupitia mabao ya Antoine Semenyo na Rodri. Forest walirejea mchezoni kupitia bao la Morgan Gibbs-White kisha dakika ya 76 Elliot Anderson aliwanyamazisha mashabiki ugani Etihad kwa kufunga bao kali.

Mechi hiyo ikielekea kukamilika, City walipiga kambi kwenye kijisanduku cha Nottingham na nusura Savinho afunge kwa shuti ya mwisho ya mchezo lakini mpira ukaondolewa kwenye laini ya goli na Murillo.

Arsenal baada ya mechi 30 ina alama 67 huku City katika mitanange 29 ikiwa na alama 60. Kizungumkuti ni kwamba Arsenal bado lazima izuru Etihad mnamo Aprili 19, mechi ambayo imefasiriwa itaamua mshindi wa taji la EPL msimu huu.

“Ni vigumu sana kuja hapa na kupata ushindi na ni dhahiri kwamba timu yoyote inayokuja hapa inateseka. Ilibidi tucheze kwa tahadhari ili kuwahi ushindi,” akasema Arteta.

“Tumekuwa tukishiriki mechi ngumu ambazo zina kasi na wachezaji wangu wanajituma sana kwenye mechi hizo. Tulifanya mazoezi na nimefurahi tumekuja hapa na kupata ushindi,” akaongeza Arteta.

City walitawala mchezo dhidi ya Forest na walikuwa wakilenga ushindi wao watano mfululizo ila walionekana kulemewa na hisia na masikitiko baada ya kipenga cha mwisho.

“Bado zimebaki mechi nyingi na lazima tucheze nao. Sasa ni Newcastle kwenye FA na hiyo ndiyo mechi nafikiria,” akasema Guardiola.

“Iwapo ni kutathmini mchezo huu basi ukweli ni kwamba tulicheza vizuri ila kuna sehemu ambazo lazima tuimarike,” akaongeza.

Vita vya kumaliza nafasi tano za kwanza na kufuzu Klabu Bingwa Ulaya navyo vinaendelea kuwa vigumu Manchester United ikichapwa kwa mara ya kwanza chini ya Kaimu Kocha Michael Carrick.

United walipoteza 2-1 kwa Newcastle United ambayo ilikuwa na wachezaji 10 uwanjani.

William Osula alitoka benchi na kufunga bao hilo dakika za jioni kwa vijana wa Eddie Howe.

Newcastle walipata pigo baada ya Jacob Ramsey kulishwa kadi ya pili ya manjano dakika ya 45.

Katika muda wa ziada wa kipindi cha kwanza, Anthony Gordon alifunga penalti na kuwapa Newcastle uongozi lakini Casemiro akajibu kwa kufungwa kwa kichwa kabla ya kipenga cha mapumziko kupulizwa.

“Newcastle walistahili ushindi na tunahitaji kujiandaa vyema zaidi kwa mechi inayokuja,” akasema Kocha wa Man United Michael Carrick.

United wapo nafasi ya tatu kwa alama 51 sawa na Aston Villa ambao walinyeshewa 4-1 na Chelsea. Joao Pedro aliyafunga magoli matatu huku Chelsea wakipita Liverpool na kuwa nafasi ya tano kwa alama 48.

West Ham United waliendelea kupambana kutoka eneo hatari la kushushwa ngazi kupitia ushindi wa 1-0 dhidi ya Fulham. Crysencio Summerville alifunga bao hilo.