Dimba

Ivory Coast kutoana kijasho na Norway Morocco wakivaana na Uholanzi raundi ya 32 Kombe la Dunia

Na TOTO AREGE June 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UWANJA wa Dallas utashuhudia pambano kali la hatua ya 32 Bora ya Kombe la Dunia usiku leo, ambapo Ivory Coast itavaana na Norway ikisaka tiketi ya kuingia 16 Bora.

Ivory Coast, maarufu kama Les Elephants, ilimaliza ya pili Kundi E nyuma ya Ujerumani, huku Norway ikifuzu kama mshindi wa pili wa Kundi I nyuma ya Ufaransa.

Chini ya kocha Emerse Fae, Ivory Coast imefuzu hatua hii kwa mara ya kwanza katika historia yake na sasa ina nafasi ya kuendelea kuweka rekodi mpya.

Les Elephants waliingia kwenye fainali hizi wakiwa na ushindi wa mechi nne mfululizo, kabla ya kuanza kampeni yao kwa kuifunga Ecuador 1-0.

Baadaye walipoteza 2-1 dhidi ya Ujerumani licha ya Franck Kessie kuipa timu hiyo bao la kuongoza kipindi cha kwanza. Mjerumani Deniz Undav aliyeingia akitokea benchi alifunga mabao mawili na kuigeuzia timu yake mchezo.

Katika mechi yao ya mwisho ya makundi, Nicolas Pepe alifunga mabao mawili na kuiwezesha Ivory Coast kuichapa Curacao 2-0, ushindi uliowapa nafasi ya kumaliza wa pili kundini.

Kwa upande wa Norway, timu hiyo imerejea Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1998 na imeongozwa na mshambuliaji Erling Haaland.

Ivory Coast huenda ikamkosa beki Wilfried Singo ambaye bado anauguza jeraha la msuli, huku Norway ikisubiri taarifa za beki Julian Ryerson aliyekosa mazoezi kutokana na maumivu ya paja.

Katika mechi nyingine ya hatua ya 32 Bora itakayopigwa katika uwanja wa Gillette, Marekani Uholanzi itachuana na Morocco katika moja ya pambano yanayosubiriwa kwa hamu kubwa.

Uholanzi iliongoza Kundi F kwa alama saba baada ya kutoka sare ya 2-2 na Japan kabla ya kuzifunga Uswidi na Tunisia.

Kikosi cha Ronald Koeman tayari kimefunga mabao 10 katika mashindano haya na kinaonekana kuwa miongoni mwa timu zinazoweza kutwaa ubingwa.

Kwa upande wa Morocco, Atlas Lions walimaliza wa pili Kundi C nyuma ya Brazil kwa tofauti ya mabao baada ya kukusanya alama saba.

Walitoa sare ya 1-1 dhidi ya Brazil kabla ya kuifunga Scotland 1-0 na Haiti 4-2, matokeo yaliyowapa tiketi ya kucheza hatua ya mtoano.

Historia pia iko upande wa Morocco baada ya kufika nusu fainali ya Kombe la Dunia mwaka 2022, mafanikio makubwa zaidi kuwahi kuyapata.