Makala

Madiwani walilia misaada kwa familia 120,000 zinazomalizwa na njaa Turkana

Na SAMMY LUTTA March 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MADIWANI katika Kaunti ya Turkana wameeleza wasiwasi kuhusu kile walichokitaja kuwa ukosefu wa usawa serikali inapokabiliana na ukame unaoathiri wadi zote 30 za kaunti hiyo, ambayo kwa sasa iko katika kiwango cha tahadhari.

Kupitia hoja ya kuahirisha kikao, madiwani walisema zaidi ya familia 120,000 zinahitaji msaada wa dharura kutokana na uhaba mkubwa wa chakula katika eneo hilo.

Wakazi wa maeneo ya mbali yaliyoathiriwa na ukame hawajapokea chakula cha msaada kutokana na changamoto za usafirishaji, licha ya serikali kusisitiza kuwa ina akiba ya kutosha kuzuia vifo vinavyotokana na njaa.

Vijiji vya Lokipoto, Nakitongo na Kibish vimetajwa kuathirika zaidi, huku wazee, watoto na watu wanaoishi na ulemavu wakisubiri msaada ambao haujawafikia kwa sababu ya vikwazo vya usafirishaji na urasimu.

Diwani wa Lokichar, Bw Samwel Lomodo, alisema baadhi ya vijiji katika wadi yake havijapokea msaada wowote.

Alionya kuwa ukame umesababisha uhaba mkubwa wa maji, kupungua kwa malisho, vifo vya mifugo, ukosefu wa chakula na kuongezeka kwa utapiamlo miongoni mwa watoto na makundi yaliyo kwenye hatari.

Alisema hali hiyo inaweza kugeuka kuwa janga la kibinadamu linaloathiri masomo, afya ya umma na uthabiti wa kijamii na kiuchumi.

Katika kongamano la wadau lililofanyika Lodwar na kuhudhuriwa na viongozi wa eneo, maafisa wa serikali na mashirika ya kibinadamu, Waziri Geoffrey Ruku, alielezwa kuwa baadhi ya manaibu makamishna wa kaunti, wamelazimika kuuza sehemu ya chakula cha msaada ili kukodisha malori ya kukisambaza.

Wabunge wa Turkana Magharibi na Turkana Kaskazini, Daniel Epuyo na Ekwom Nabuin, walieleza changamoto zinazochelewesha misaada wakitaja ukosefu wa fedha za kusafirisha chakula hadi vijiji vya mbali.

Maeneo ya Kibish yaliyo takriban kilomita 400 kutoka Lodwar yameripotiwa kukosa misaada kabisa, huku wafugaji wanaovuka mipaka ya Uganda, Ethiopia na Sudan Kusini wakisahaulika.

Afisa anayesimamia majanga katika Kaunti ya Turkana, Bw Patrick Losike, aliambia kamati ya Bunge la Kaunti kuwa kufikia Jumatano, wadi 22 zilikuwa zimepokea chakula cha msaada, huku zingine zikitarajiwa kupokea ndani ya siku nane. Alitaja changamoto za usafirishaji na wakandarasi kushindwa kuwasilisha chakula kwa wakati.

Diwani maalum, Bi Mary Nakwapwan, alikosoa kucheleweshwa kwa misaada, akisema mifugo wamekonda na familia nyingi, hata mjini Lodwar, hukaa siku kadhaa bila mlo.

Alisisitiza haja ya miradi endelevu kama visima vinavyofanya kazi na mipango ya unyunyizaji.

Afisa wa Kaunti anayesimamia Kilimo na Mifugo Michael Eregae, alisema vifo vya mifugo vimefikia asilimia 10.

Alithibitisha mlipuko wa ugonjwa unaoathiri mbuzi na kondoo, huku kukiwa na mpango wa kuchanja mifugo 600,000.

Licha ya hatua hizo, madiwani wanasisitiza kuwa uratibu wa haraka na uwekezaji wa muda mrefu ni muhimu kuzuia majanga ya mara kwa mara ya ukame katika kaunti hiyo iliyo miongoni mwa zilizo hatarini zaidi kutokana na mabadiliko ya tabianchi nchi.