Aliyesajili ‘Linda Mwananchi Party’ apuuza malalamishi ya Sifuna na wenzake
MZOZO kuhusu umiliki na usajili wa chama kinachopendekezwa cha Linda Mwananchi Party of Kenya umeanza kuchukua mkondo wa kisheria baada ya aliyewasilisha jina hilo, kupinga rasmi malalamishi yaliyowasilishwa na kundi la viongozi wa ODM wanaotaka kuzuia usajili wake.
Kupitia mawakili wake, Bw Charles Wanyonyi, aliyewasilisha ombi la kuhifadhi jina la Linda Mwananchi Party of Kenya, amepuuza pingamizi iliyowasilishwa na kundi linaloegemea upande wa Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna, akisema halina msingi wa kisheria.
Katika barua kwa Afisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP), mawakili wa Bw Wanyonyi walisema mteja wao alitumia haki yake ya kikatiba kama Mkenya kuomba kusajili chama na hakuwa akimtumikia kiongozi yeyote wa kisiasa.
Pingamizi hiyo iliwasilishwa na mawakili kwa niaba ya Bw Sifuna na viongozi wengine akiwemo Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi na Seneta wa Kisii Richard Onyonka.
Pia wabunge Babu Owino (Embakasi Mashariki), Caleb Amisi, Anthony Kibagendi, Majimbo Kalasinga, Caroli Omondi na Barongo Obadiah wanawaunga mkono.
Viongozi hao wanadai kuwa kauli mbiu ya “Linda Mwananchi” imehusishwa kwa karibu na mikutano yao ya kisiasa na harakati za kuwahamasisha wananchi, hivyo kuisajili kama chama bila ushiriki wao kunaweza kupotosha umma na kusababisha mkanganyiko kuhusu umiliki na mwelekeo wa vuguvugu hilo.
Aidha, wameonya kuwa watuwanaohusika na chama hicho wanaweza kutumia majina yao na umaarufu wao wa kisiasa kukusanya fedha kwa njia isiyo halali.
Hata hivyo, mawakili wa Bw Wanyonyi wamesema jina hilo halijawahi kusajiliwa rasmi na mtu au taasisi yoyote kama chama cha kisiasa, hivyo hakuna mtu mwenye haki ya kipekee kulihusu.
Wameeleza kuwa Kifungu cha 8 cha Sheria ya Vyama vya Kisiasa kinaeleza sababu pekee zinazoweza kumfanya Msajili kukataa jina, kama vile kufanana na chama kingine kilichosajiliwa au kuwa kinyume na maslahi ya umma – hoja ambazo, kwa mujibu wao, hazijatimizwa.
Mzozo huo sasa umeiweka afisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa, inayoongozwa na Bw John Cox Lorionokou, katika hali tete ya kufanya uamuzi wa kisiasa na kisheria.
Kisheria, Msajili ana siku 14 kuchunguza ombi la kuhifadhi jina la chama.
Wakati huo huo, Mwenyekiti wa Kitaifa wa ODM, Bi Gladys Wanga amewataka wanachama wa Linda Mwananchi kueleza wazi iwapo wanakusudia kubaki ndani ya chama au kuanzisha mwelekeo wao huru.
Mbunge wa Homa Bay Mjini, Bw Peter Kaluma, hata hivyo, amesisitiza kuwa ODM bado iko imara.
Wachambuzi wanasema mvutano huo unaonyesha umuhimu wa chapa ya kisiasa katika mazingira ya ushindani kuelekea 2027.
Wanakumbusha kuwa kabla ya kura ya maoni ya 2005, jina la ODM liliwahi kusajiliwa na Mugambi Imanyara kabla ya baadaye kutwaliwa na marehemu Raila Odinga.
Hatima ya Linda Mwananchi sasa iko mikononi mwa Msajili, huku ombi hilo likisubiri uamuzi rasmi.