Habari

Kamati yapinga mswada wa kudhibiti nauli za matatu

Na SAMWEL OWINO August 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KAMATI ya Bunge kuhusu Uchukuzi na Miundombinu imependekeza wabunge wakatae kabisa Mswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi na Usalama Barabarani (NTSA), ikisema kudhibiti nauli za magari ya uchukuzi wa umma kunaweza kusababisha matatizo makubwa kuliko manufaa.
Katika ripoti iliyowasilishwa bungeni, kamati ilisema Kenya inaendeshwa kwa mfumo wa uchumi wa soko huru, na hivyo serikali haipaswi kuingilia nauli za matatu kwa njia ya sheria.
Kamati ilionya kuwa utekelezaji wa sheria hiyo utakumbwa na changamoto za kiutawala na ufuatiliaji, huku ukikinzana na baadhi ya makubaliano ya kikanda na kimataifa ambayo Kenya imetekeleza.
Kamati ilieleza kuwa sekta ya uchukuzi wa umma inaendeshwa zaidi na wawekezaji wa kibinafsi kupitia vyama vya akiba na mikopo (Sacco), kampuni na watu binafsi. Kwa sababu hiyo, kudhibiti nauli kutahitaji mashauriano ya kina kutokana na gharama zinazobadilika mara kwa mara, ikiwemo bei ya vipuri vinavyoagizwa kutoka nje ya nchi.
Mswada huo wa mwaka 2023 unalenga kurekebisha Sheria ya NTSA ya mwaka 2012 ili kuweka mwongozo wa serikali kuhusu nauli zinazotozwa abiria wa magari ya uchukuzi wa umma.
Mswada huo, unaodhaminiwa na Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa, unapendekeza kukomesha uhuru ambao wamiliki wa matatu wamekuwa nao wa kuamua nauli wanavyotaka, hasa wakati wa sikukuu, mvua au misimu ya shughuli nyingi.
Iwapo utapitishwa, Kenya itaungana na mataifa kama Ghana, Rwanda, Tanzania, Cameroon na Ujerumani ambako serikali hushiriki katika kuweka kiwango cha chini cha nauli za usafiri wa umma.
Hata hivyo, aliyekuwa Waziri wa Uchukuzi Kipchumba Murkomen alipinga mswada huo alipofika mbele ya kamati mwaka 2023. Alisema Kenya iliondoa sera za kudhibiti bei kuanzia mwishoni mwa miaka ya 1980 hadi 1990 baada ya mageuzi ya kiuchumi yaliyolenga kupatia nguvu zaidi soko huru kuliko serikali.
Kwa upande wake, Shirikisho la Sekta ya Uchukuzi wa Umma pia limepinga mswada huo likisema kabla ya serikali kuanza kuamua nauli, ni lazima iweke sera, sheria na taasisi madhubuti zitakazowezesha mfumo huo kufanya kazi.
Shirikisho hilo lilibainisha kuwa gharama kubwa zinazowakabili waendeshaji wa matatu tayari zinadhibitiwa na sheria. Mafuta hudhibitiwa na Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA), bima husimamiwa na Mamlaka ya Kudhibiti Bima (IRA), huku waendeshaji wakitakiwa kutii sheria za ajira, kujiunga na Sacco au kampuni, kulipa ada za kaunti, kufanya ukaguzi wa magari kila mwaka na kuwa na vifaa vya usalama.
Kwa mujibu wa shirikisho hilo, masharti hayo yote huongeza gharama za uendeshaji na kufanya biashara ya matatu kuwa ngumu, huku kampuni nyingi zikifungwa baada ya miaka michache.
Lilisema sekta hiyo inapaswa kuendelea kufanya kazi katika mazingira ya ushindani wa soko huru kama ilivyo kwa mashirika ya ndege, ambayo hubadilisha nauli kulingana na msimu, likizo za shule, Pasaka na Krismasi.
Licha ya mapendekezo ya kamati, Bw Barasa alisema hatarudi nyuma. Alisisitiza kuwa uamuzi wa mwisho utatolewa na Bunge.
“Nimeona ripoti ya kamati ikitaka mswada ukataliwe, lakini ni Bunge litakaloamua hatima yake,” alisema.
Mjadala kuhusu mswada huo ulianza wiki hii na unatarajiwa kuendelea wiki ijayo, huku wabunge wengi wakionekana kuunga mkono hatua ya kuweka utaratibu wa kudhibiti ongezeko la ghafla la nauli za matatu.
Si mara ya kwanza pendekezo kama hilo kujitokeza. Mwaka 2018, Bunge lilikataa mpango wa Wizara ya Uchukuzi uliolenga kumpa waziri mamlaka ya kuweka nauli za magari ya uchukuzi wa umma. Vilevile mwaka 2020, Chama cha Wamiliki wa Matatu kilipinga pendekezo kama hilo.