Siasa sasa zapelekwa WhatsApp uchaguzi wa 2027 ukikaribia
KATIKA siasa za Kenya za sasa, mapambano makali hayafanyiki tena kwenye mikutano ya hadhara, Bunge au runinga pekee. Sasa vita hivyo vimechacha kwenye makundi ya WhatsApp.
Makundi yaliyoundwa awali kwa ajili ya kuratibu shughuli na kuhamasisha wafuasi sasa yamegeuka kuwa uwanja wa kupimana nguvu, kujenga au kuvunja ushirikiano na kuonyesha uaminifu wa kisiasa.
Kuongezwa, kuondolewa au hata kuzimwa kwenye kundi sasa ni ujumbe wa kisiasa unaoweza kuzua mjadala mkubwa.
Hapo awali, wanaoasi walikuwa wakifukuzwa kutoka afisi za vyama au kuzuiwa kuhudhuria mikutano. Leo, hatua hiyo hufanyika kwa kubofya kitufe cha kuwaondoa kwenye kundi la WhatsApp.
Aidha, makundi hayo yamekuwa mahali pa mijadala mikali kuhusu misimamo ya vyama.
Baadhi ya mapendekezo huzimwa humo kabla hata hayajafika bungeni, huku mengine yakianza kama mjadala wa WhatsApp na baadaye kuibuka kwenye mijadala ya Seneti na Bunge la Kitaifa.
Mvutano unaoendelea ndani ya ODM kati ya viongozi wa mrengo wa Linda Mwananchi na uongozi wa chama unaendelezwa kwa kiasi kikubwa kupitia makundi hayo.
Wiki iliyopita, wabunge wanaohusishwa na mrengo huo waliondolewa kwenye kundi la WhatsApp la Kundi la Wabunge wa ODM, ambalo hutumika kupanga ajenda za chama na kuelekeza wabunge jinsi ya kupiga kura au kujadili miswada.
Walioondolewa ni pamoja na Maseneta Edwin Sifuna wa Nairobi, Godfrey Osotsi wa Vihiga na Richard Onyonka wa Kisii.
Wabunge Babu Owino, Caroli Omondi, Caleb Amisi, Anthony Kibagendi, Clive Gisairo na Wilberforce Oundo pia walitimuliwa kwenye kundi hilo.
Bw Sifuna alisema baada ya mkutano wa kisiasa Kitale waligundua wameondolewa kwenye kundi hilo, hatua aliyofasiriwa kama ishara kwamba uongozi wa ODM hauwataki tena.
Kwa upande wake, Seneta Osotsi alisema hii si mara ya kwanza kwao kufutwa kwenye makundi ya chama.
Alikumbuka kuwa mapema mwaka huu baadhi yao waliondolewa kwenye kundi la Baraza Kuu la Kitaifa (NEC) kabla ya kupokonywa nyadhifa za chama.
Alisema hatua hiyo inaonyesha kuwa wameonekana kama watu wasiostahili kuwa ndani ya ODM na sasa wanatafakari kusitisha michango yao ya kila mwezi kwa chama.
Mivutano hiyo pia ilijitokeza wakati wa kuondolewa kwa Bw Sifuna kama Naibu Kiranja wa Wachache katika Seneti. Taarifa ya mkutano ilitumwa kupitia WhatsApp, jambo lililosababisha mabishano makali kabla ya mkutano huo kugeuka vurugu.
Hata hivyo, tukio lililovuta hisia zaidi lilikuwa kuondolewa kwa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kwenye kundi la WhatsApp la Ikulu wakati wa tofauti zake na Rais William Ruto.
Bw Gachagua alisema yeye, katibu wake binafsi na mkuu wa wafanyakazi wake waliondolewa kwenye kundi hilo, hatua iliyowafanya washindwe kupata taarifa kuhusu ratiba ya Rais na shughuli rasmi za Ikulu. Muda mfupi baadaye aling’olewa mamlakani kupitia mchakato wa kumbandua.
Mbunge wa Embakasi Central Benjamin Gathiru, maarufu kama Mejja Donk, alisema wabunge wengi wanaoonekana kumuunga mkono Bw Gachagua pia wameondolewa kwenye makundi ya Kenya Kwanza na UDA.
Anasema hatua hiyo imewanyima taarifa za mikutano ya chama na shughuli nyingine za kisiasa. Kwa sababu hiyo, amesema alipunguza mchango wake wa kila mwezi kwa chama kutoka Sh20,000 hadi Sh500.
Kwa mujibu wa wanasiasa mbalimbali, makundi ya WhatsApp sasa ni nyenzo muhimu katika kampeni za uchaguzi.
Hutumika kupanga mikutano ya kisiasa, kuajiri wahudumu wa kujitolea, kusambaza ratiba za kampeni na kueneza ujumbe kwa wafuasi.
Lakini pamoja na manufaa hayo, makundi hayo pia yamegeuka njia ya ujasusi wa kisiasa.
Wapinzani hujiingiza kwenye makundi hayo na kutoa mikakati ya siri kwa hasimu wao.
Katika kitabu chake Unwritten Political Rules, Cathy Irungu anaeleza jinsi watu waliodaiwa kuwa vibaraka walivyopenya kwenye timu ya kampeni ya Raila Odinga mwaka 2022 na kupata taarifa muhimu kupitia makundi ya WhatsApp.
Na kadiri uchaguzi mkuu wa 2027 unavyokaribia, WhatsApp inatarajiwa kuendelea kuwa silaha muhimu ya kisiasa.
Hata hivyo, wachambuzi wanaonya kuwa jukwaa hilo pia linaongeza kasi ya kusambaa kwa habari za uongo, kauli za kughushi na video zilizohaririwa ambazo zinaweza kupotosha umma.
Wachambuzi wa siasa wanasema matumizi ya WhatsApp yamebadili kabisa namna vyama vya kisiasa vinavyofanya maamuzi.
Tofauti na zamani ambapo viongozi walilazimika kukutana ana kwa ana ili kujadili masuala muhimu, sasa maamuzi mengi hufanyika kupitia simu za mkononi.
Mikutano ya dharura hupangwa ndani ya dakika chache, huku taarifa zikisambazwa kwa mamia ya wanachama kwa wakati mmoja.
Hata hivyo, kasi hiyo imeambatana na changamoto nyingi.
Ujumbe unaovuja kutoka kwenye makundi ya viongozi mara nyingi huzua mizozo ya kisiasa na kuwapa wapinzani nafasi ya kufahamu mikakati ya vyama.
Wakati mwingine picha za mazungumzo ya siri husambazwa mitandaoni na kusababisha viongozi kulaumiana kwa usaliti au kuvuja kwa taarifa.
Kutokana na hali hiyo, baadhi ya vyama sasa vimeweka masharti makali kuhusu matumizi ya makundi ya WhatsApp.
Wanachama wanaotuhumiwa kuvuja siri au kupinga maamuzi ya chama huondolewa kwenye makundi hayo au kunyamazishwa wasichangie mijadala.
Hatua hizo zimegeuza WhatsApp kuwa chombo chenye ushawishi mkubwa katika siasa za kisasa, ambapo kubaki au kuondolewa kwenye kundi kunaweza kufasiriwa kama ishara ya kupanda au kushuka kwa ushawishi wa mwanasiasa ndani ya chama chake.