Jumwa auza sera za UDA miezi michache baada ya kutangaza amejiunga na PAA
MIEZI miwili baada ya aliyekuwa waziri wa masuala ya Jinsia, Aisha Jumwa kutangaza kuwa amehama chama cha UDA na kujiunga na chama kinachohusishwa na Spika wa Seneti, Amason Kingi, Pamoja African Alliance (PAA), mwanasiasa huyo amewaacha wengi na maswali baada ya kendeleza mikutano yake akiuza sera za UDA.
Kwa muda wa wiki mbili zilizopita, Bi Jumwa amefanya mikutano mbalimbali akivalia sare za UDA na kusifu uongozi wa Raisi William Ruto na Naibu wake Kithure Kindiki hivyo kukanganya wafuasi wake na kuwaacha na maswali mengi kuhusiana na karata zake za 2027.
Waziri huyo wa zamani ambaye alitangaza mwezi wa Disemba mwaka jana kuhama chama cha UDA kwa madai ya kutengwa na viongozi wakuu serikalini, anaonekana kuwekeza kwa vyama hivyo viwili, ikizingatiwa UDA tayari imechagua aliyekuwa Spika wa kaunti ya Kilifi Jimmy Kahindi kupeperusha bendera ya ugavana ya UDA mwaka ujao.
Bi Jumwa katika mkutano wake wiki hii alisema ataendelea kukutana na viongozi wa mashinani wa chama cha UDA ili kwa pamoja kushauriana, kutathmini tuwalipotoka, walipo sasa, na kupanga kwa umoja mahali wanaelekea.
“Tunaamini kuwa nguvu ya chama na maendeleo ya jamii huanzia mashinani. Ndiyo maana sauti ya wananchi na uongozi wa mashinani ni nguzo muhimu katika kujenga mustakabali imara wa Kilifi yetu na Nchi kwa jumla,” alisema Bi Jumwa.
Kuondoka kwa waziri huyo wa zamani UDA kulitajwa kama pigo kubwa na iwapo wangeendeleza muungano katika PAA pamoja na wakili George Kithi, gavana wa sasa wa kaunti ya Kilifi Gideon Mung’aro angekuwa na kibarua kigumu kuhifadhi kiti hich cha ugavana.
Katika uchaguzi wa ugavana wa 2022, Bi Jumwa alipata kura 65,893 huku Bw Kithi alipata kura 64,329 dhidi ya Bw Mung’a ro ambaye aliibuka mshindi kwa kura 143,773.
Licha ya Bi Jumwa kuendeleza kampeni za UDA, atakuwa na kizungumkuti siku za usoni kwani Katibu mkuu wa UDA Hassan Sarai alisema mwaka wa 2027 kila chama kitawakilisha mgombeaji wake na tayari Bw Kahindi alituma maombi kuwa mgombeaji wa ugavana Kilifi kwa tiketi ya UDA.
“Kutokana na kuondoka kwa Bi Jumwa, tumemuteuwa Bw Kahindi kuongoza chama hicho Kilifi na baadaye kumuunga mkono kuwania kiti cha ugavana,” alisema Bw Omar.
Katika uchaguzi mdogo wa Magarini Novemba mwaka jana, chama cha UDA na PAA waliungana na kuunga mkono mgombeaji wa ODM Harry Kombe ambaye aliebuka mshindi dhidi ya mgombeaji wa DCP Stanely Kenga.
Bw Kahindi alihama ODM mwaka wa 2022 baada ya chama hicho kuteuwa Bw Mung’aro kama mgombeaji wake was gavana badala yake na kuungana na Jumwa kufanyia Raisi Ruto kampeni.
Bw Kahindi alihama ODM mwaka wa 2022 baada ya chama hicho kuteuwa Bw Mung’aro kama mgombeaji wake was gavana badala yake na kuungana na Bi Jumwa kufanyia Raisi Ruto kampeni.
Kabla ya Bi Jumwa kuelekea PAA mwisho wa mwaka jana, alisema aliona heri kuhamia chama kinachohusishwa na wenyeji anapolenga azma yake ya kumng’oa gavana wa sasa Bw Mung’aro.
“Wanasiasa kuhama chama ni jambo la kawaida hata Raisi Ruto amefanya hivyo mara kadhaa. Hata hivyo, chama cha PAA kiko kwa serikali na hakuna kosa lolote limefanyika,” alisema Bi Jumwa.
“Nilibaki na maswali kuhusu kwa nini Raisi Ruto hakuongelea cha UDA alipokuwa huku. Nilionelea kujiunga na PAA ambacho ni moja wa chama tanzu serikalini,” alisema Bi Jumwa.
Hata hivyo Bi Jumwa alionekana kuwa shupavu bila kujutia kuondoka kwa chama tawala akisema bado PAA kiko serikalini na kubadili mienendo yake kupigia debe UDA tena kumeacha wengi na maswali.
Kinyang’anyiro hicho kinatarajiwa kuwa kigumu kwani gavana wa sasa Bw Mung’aro anatarajiwa kutetea kiti hicho ilikumaliza mihula miwili.