Habari

‘PAWA’: Ruto, Oburu kuunda kikosi cha kusuka ndoa 2027

Na MOSES NYAMORI Na JUSTUS OCHIENG March 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto na kiongozi wa ODM Oburu Oginga Machi 9, 2026 wanatarajiwa kutoa ramani ya kina kuhusu muungano wa kisiasa wanaosuka kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.
Habari zinaonyesha kuwa mkutano wa pamoja wa Kundi la Wabunge wa chama tawala UDA na ODM utakaofanyika katika Nairobi utakuwa jukwaa muhimu la kupiga hatua kubwa kuelekea kuunda muungano wa kusaidia Rais Ruto kupata muhula wa pili madarakani.
Hata hivyo, mrengo unaohusishwa na Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna umekosoa mkutano huo vikali na kuutaja kama usaliti mkubwa kwa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga.
Kupitia naibu kiongozi wa chama Godfrey Osotsi, kundi hilo limesema kuwa kuendelea kujadiliana kuhusu muungano na UDA wakati vipengele vingi vya ajenda ya mageuzi havijatekelezwa ni hatua inayolenga maslahi ya kisiasa ya baadhi ya viongozi wa ODM.
Taarifa zaidi zinaonyesha kuwa suala la kutenga maeneo ya kisiasa linaibuka kama mojawapo ya hoja tata katika mazungumzo ya muungano. UDA imepinga mpango huo, lakini ODM inasisitiza kuwa kila chama kinapaswa kulindwa katika ngome zake ili kuepusha ushindani wa ndani unaoweza kugawa kura na kuwafaidi wapinzani.
Kiongozi wa wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohammed alisema ODM inapendekeza mfumo uliotumika katika chaguzi ndogo za Novemba 27, 2025. Katika chaguzi hizo, ODM ilisimamisha wagombea katika maeneo ya Ugunja, Kasipul na Magarini huku UDA ikiwania viti vya Mbeere North, Baringo na Malava.
“Kwa nini tuwe na mpangilio huo katika chaguzi ndogo lakini tusitumie katika uchaguzi mkuu? Huo ndio mfumo tunaotaka utekelezwe katika uchaguzi wa 2027,” alisema Mohammed.
Mohammed pamoja na Kiongozi wa walio wengi bungeni Kimani Ichung’wah walituma mialiko kwa wabunge wa Kenya Kwanza na ODM kuhudhuria mkutano huo ambao pia utaadhimisha mwaka mmoja tangu kutiwa saini kwa mkataba kati ya Rais Ruto na Raila Odinga Machi 7, 2025.
Katika ujumbe kwa wabunge, Ichung’wah alisema mkutano huo utapitia ripoti ya utekelezaji wa ajenda ya vipengele 10 iliyokubaliwa katika makubaliano hayo pamoja na kujadili athari za sera na masuala mengine ya kitaifa ndani ya mfumo wa ushirikiano wa kisiasa.
Kwa mujibu wa Mohammed, Rais Ruto na Oburu Oginga watatumia mkutano huo kutangaza ramani ya mazungumzo ya muungano, ikiwemo kutaja timu za mazungumzo kutoka kila upande zitakazoongoza mchakato wa kuunda muungano huo kuelekea uchaguzi wa 2027.
“Tutatoa tangazo muhimu litakalosukuma mbele mazungumzo kati ya UDA na ODM. Ramani kamili itawekwa ikionyesha hatua zote tutakazochukua kuelekea uchaguzi wa 2027,” alisema mbunge huyo wa Suna Mashariki.
Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi pia alidokeza kuhusu mpango huo, akisema wakosoaji wa mpango huo watajikuta wakitengwa kadri muungano huo wa kabla ya uchaguzi utakavyoundwa.
“Hatua ya mkutano wa kundi la wabunge ni sahihi na itawaumbua wale waliokuwa wakipinga mpango huu. Safari ya kuelekea uchaguzi wa 2027 sasa inaanza rasmi,” alisema Wandayi.
Viongozi wakuu wa UDA na ODM tayari wamempa Rais Ruto na Oburu Oginga mamlaka ya kuanza mazungumzo rasmi ya muungano. ODM pia imeashiria kuwa iko tayari kumuunga mkono Rais Ruto kwa muhula wa pili, lakini imeweka wazi kuwa wadhifa wa Naibu Rais ni mojawapo ya matakwa yake muhimu. Kwa sasa kiti hicho kinashikiliwa na Kithure Kindiki.