Mudavadi kula hu wabunge wakikataa Sh1.15 bilioni alizoomba
WABUNGE wamekataa kuidhinisha fedha zaidi kwa ukarabati na uboreshaji wa jengo lililokodishwa kutumika kama afisi ya Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi katika makao makuu ya Shirika la Reli Nchini (KRC).
Hatua hiyo inajiri wiki moja tu baada ya kufichuka kuwa bajeti ya Ikulu ya Rais ya mwaka wa kifedha wa 2025/2026 ilipanda maradufu hadi Sh16.998 bilioni baada ya kutengewa pesa zaidi kupitia mwanya uliotolewa chini ya Kipengele cha 23 cha Katiba.
Afisi ya Mudavadi ilikuwa imeomba Sh1.15 bilioni zaidi kufadhili utoaji wa huduma shirikishi na zile za usimamizi, pamoja na ukarabarati wa jengo linalotumika na maafisa wake katika makao makuu ya KRC
Stakabadhi zilizowasilishwa bungeni zinaonyesha kuwa afisi hiyo hulipa kodi ya Sh106 milioni kila mwaka kutumia jengo hilo na imetumia jumla ya Sh363 milioni kwa ukarabati tangu 2023.
Wiki jana wabunge waliidhinisha mapendekezo ya Kamati ya Bunge kuhusu Bajeti (BAC) kuwa pesa hizo (Sh1.15 bilioni) ni nyingi zaidi na haziwezi kutumika kukarabati jengo ambalo halimilikiwi na wizara bali imekodishwa.
Hata hivyo, kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Alego Usonga Samuel Atandi iliungama kuwa jengo hilo liko katika hali mbaya na linafaa kufanyiwa ukarabati ili liwekwe mitambo ya usalama, miundomsingi ya ICT na vifaa vingine vya kurahisisha utendakazi.
Badala yake wanachama wa kamati hiyo waliitengea afisi ya Mudavadi Sh827 milioni pekee za matumizi ya kawaida katika mwaka wa kifedha wa 2026/27 huku wakikosa kutenga fedha zozote kwa matumizi ya miradi ya maendeleo.
“Fedha zaidi za umma hazitatolewa kwa ukarabati wa majengo yaliyokomeshwa kama vile afisi ya Mkuu wa Mawaziri. Hazina ya Kitaifa inapasa kukoma kutoa ufadhili kwa shughuli kama hizo,” Bw Atandi akasema kwenye ripoti aliyowasilisha bungeni.
Kamati hiyo pia ilikataa kuidhinisha mgao wa Sh623.37 bilioni zaidi kulingana na maombi yaliyowasilishwa na Wizara, Idara na Mashirika (MDAs) ya serikali kuu, ikitaja uhaba wa fedha kama sababu.
Hazina ya Kitaifa iliitengea afisi ya Mudavadi Sh556.6 milioni katika mwaka wa sasa wa kifedha na ikakadiria kuongezeka kwa mgao kwa afisi hiyo hadi Sh850.9 milioni katika mwaka ujao wa kifedha wa 2026/27.
Makisio hayo yanaonyesha kuwa bajeti ya afisi hiyo itapanda hadi 850.9 milioni katika mwaka wa kifedha wa 2027.28 na Sh875.8 milioni katika mwaka wa 2028/29.