TAHARIRI: Kampeni hizi za mapema ni kikwazo kwa amani na ustawi
KAMPENI za mapema zinazoendelea kushuhudiwa nchini ni jambo la kusikitisha ambalo linapaswa kukemewa kwa kinywa kipana.
Inapozingatiwa kuwa uchaguzi mkuu ujao umesalia takribani mwaka mmoja na nusu, mikutano hii ya kisiasa inayochochea hisia kali na mara nyingi kuzua ghasia na hata vifo inastahili kukomeshwa.
Mwenendo huu si kinyume tu cha msingi wa demokrasia yenye ustaarabu, bali pia ni tishio kwa amani, uchumi na mshikamano wa kitaifa.
Japo ghasia katika mikutano ya kisiasa si jambo jipya nchini, tukio la majuma matatu yaliyopita katika eneo la Kitengela, Kaunti ya Kajiado, ni ishara ya hali hatari katika uchaguzi ujao.
Katika tukio hilo la kusikitisha, makanika Michael Oyamo alipoteza maisha baada ya kupigwa risasi wakati polisi wakiingilia mkutano wa vuguvugu la Linda Mwananchi ulioongozwa na Seneta Edwin Sifuna, Mbunge Babu Owino na Gavana James Orengo.
Kifo hicho ni ishara ya hatari inayotukabili iwapo wanasiasa wataendelea kuchochea mikutano ya mapema iliyojaa hisia kali na mvutano wa kisiasa.
Ni bayana kuwa kampeni za mapema zina madhara mengi kuliko manufaa kwa taifa.
Kwanza, zinadhoofisha juhudi za kukuza uchumi wa nchi.
Wananchi wengi wanaohudhuria mikutano hiyo hutumia muda mwingi katika shughuli za kisiasa badala ya kushiriki katika kazi za uzalishaji kama vile biashara, kilimo na ujasiriamali.
Katika kipindi hiki ambacho taifa linapambana na changamoto za kiuchumi, ni muhimu wananchi wajikite katika shughuli za kujenga uchumi badala ya kushiriki katika siasa.
Aidha, kampeni hizi za mapema zinanyonya rasilimali za umma. Wanasiasa, hasa wale walio serikalini, hutumia pesa nyingi kuendesha mikutano hiyo.
Gharama za usafiri wa maafisa wa serikali, malazi, ulinzi na hata rushwa kwa wananchi ili kuhudhuria mikutano hiyo ni mzigo kwa walipa kodi.
Badala ya fedha hizo kuelekezwa katika miradi ya maendeleo kama vile afya, elimu na miundomsingi, zinapotea katika siasa za mapema zisizo na tija.
Zaidi ya hayo, mikutano ya kisiasa ya mapema mara nyingi huambatana na hisia kali na chuki za kisiasa.
Hali hii husababisha wafuasi wa pande tofauti kuhasimiana na wakati mwingine kuzua ghasia.
Inapoongezwa na madai ya njama za kisiasa za kujaribu kuzima umaarufu wa wapinzani, matokeo yake huwa ni majeruhi na hata vifo vya wananchi wasio na hatia.
Tukio la Kitengela linapaswa kuwa funzo tosha kwa viongozi na vyombo vya dola kwamba siasa zisipoendeshwa kwa busara zinaweza kugharimu maisha ya watu.
Kwa msingi huo, ni wajibu wa wanasiasa wote kuweka mbele maslahi ya taifa kuliko tamaa zao za kisiasa.
Kampeni zina wakati wake rasmi, na wakati huo bado haujawadia.
Serikali, vyama vya siasa na taasisi za usimamizi wa uchaguzi zinapaswa kuchukua hatua madhubuti kudhibiti mikutano ya kisiasa ya mapema inayochochea ghasia.
Kenya inahitaji kipindi cha utulivu ili kujenga uchumi na kuimarisha mshikamano wa kitaifa.
Huu si wakati wa kampeni za mapema, bali ni wakati wa viongozi kufanya kazi kwa bidii kuwatumikia wananchi waliowachagua.