Tahariri

TAHARIRI: Hii Bajeti mpya kamwe haiwezi kumkomboa mwananchi

Na MHARIRI MKUU June 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAZIRI wa Fedha, John Mbadi, aliwasilisha jana bajeti ya Sh4.82 trilioni ya mwaka wa kifedha wa 2026/27 huku serikali ikijivunia kuweka mikakati ya kuendeleza uchumi, kuboresha huduma za umma na kuimarisha ustawi wa wananchi.

Hata hivyo, kuna uhalisia mchungu kwamba bajeti hiyo huenda ikawa mzigo mwingine kwa mwananchi wa kawaida ambaye tayari anahangaishwa na gharama kubwa ya maisha.

Jambo la kwanza linalotia wasiwasi ni kiwango kikubwa cha nakisi ya bajeti ambacho kitalazimisha serikali kukopa takribani Sh1.1 trilioni ili kuziba pengo la matumizi.

Kati ya fedha hizo, karibu Sh1 trilioni zinatarajiwa kukopwa katika soko la ndani huku Sh100 bilioni zikitoka masoko ya mikopo ya nje.

Hili si jambo la kupuuzwa kwa sababu linaonyesha kuwa serikali bado haijaweza kuwianisha matumizi yake na mapato inayokusanya.

Athari za ukopaji huu wa ndani ni kubwa. Serikali inapokopa kwa kiwango kikubwa kutoka kwa benki za kibiashara, taasisi hizo huona ni salama zaidi kuikopesha serikali kuliko wafanyabiashara na wawekezaji binafsi.

Matokeo yake ni kwamba sekta ya kibinafsi, ambayo ndiyo mwajiri mkuu nchini, hukosa mtaji wa kupanua biashara zake, kuanzisha miradi mipya na kuajiri wafanyakazi zaidi.

Hivyo basi, wakati serikali ikijisifu kuwa imeandaa bajeti ya kukuza maendeleo, ukweli ni kwamba inaweza kuwa inanyima uchumi nguvu zinazotokana na uwekezaji wa kibinafsi.

Katika mazingira ambapo maelfu ya vijana huingia kwenye soko la ajira kila mwaka, jambo la msingi lingekuwa kuweka mazingira yanayochochea biashara kustawi.

Hata hivyo, bajeti hii haionekani kutoa mwelekeo wa kutosha wa kuhamasisha ukuaji wa sekta binafsi.

Badala yake, inategemea zaidi matumizi ya serikali na ukopaji, mkakati ambao umeendelea kutumiwa kwa miaka mingi bila kuleta matokeo mazuri.

Aidha, wataalamu wa uchumi wamekuwa wakisisitiza kuwa njia bora ya kuchochea ukuaji ni kupunguza mzigo wa ushuru kwa wananchi na wafanyabiashara.

Kupunguza ushuru kungewaachia watu fedha zaidi za kuwekeza, kupanua biashara na kuongeza matumizi katika uchumi.

Kadiri shughuli za kiuchumi zinavyoongezeka, ndivyo serikali inavyoweza kukusanya mapato mengi zaidi kutokana na kuongezeka kwa idadi ya walipa ushuru na ukuaji wa biashara.

Ni wakati mwadaka kwa serikali kutambua kwamba maendeleo ya kweli hayatokana na ukopaji usioisha. Bajeti endelevu ni ile inayoweka mkazo katika kukuza uzalishaji, uwekezaji na ubunafu wa sekta binafsi.

Bila kufanya hivyo, mzigo wa deni utaendelea kuongezeka na mwananchi wa kawaida ndiye atakayebeba gharama kuu.

Bajeti ya mwaka huu, kwa hivyo, inastahili kuchunguzwa upya kwa jicho la tahadhari.