Dimba

Firat aombolezwa kama kocha nguli aliyefungulia Harambee Stars milango kimataifa

Na CECIL ODONGO March 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KOCHA wa zamani wa Harambee Stars Engin Firat ambaye aliaga dunia jana Uturuki, ameombolezwa kama aliyemakinikia kazi yake na mwenye taaluma pevu ambaye mchango wake kwenye soka ya Kenya hautasahaulika.

Firat aliaga dunia katika uwanja wa Istabul, akielekea nyumbani kutoka Lebanon. Klabu ya Nejmah ambayo alikuwa akiifundisha, ilithibitisha kuwa aliaga dunia kutokana na mshtuko wa ghafla wa moyo.

Alikuwa akirejea nyumbani kutoka Lebanon kutokana na vita kati ya Amerika-Israel dhidi ya Iran ambavyo vimetikisa Mashariki ya Kati.

Israel imekuwa ikishambulia Lebanon kwa makombora ikiwalenga wapiganaji wa Hezbollah.

Firat 55, alihudumu kama Kocha wa Harambee Stars kuanzia Septemba 19 2021 hadi 2024. Alijiunga na Nejmah mwezi uliopita.

“Tunatuma rambirambi zetu kwa familia na marafiki wa kocha wa zamani wa Harambee Stars Engin Firat. Mchango wake kwenye soka ya Kenya utakumbukwa sana,” akaandika Rais wa Shirikisho la Soka Nchini (FKF) Hussein Mohamed.

Naye Makamu Rais wa FKF MacDonald Mariga aliandika “Ahsante sana kwa mchango wako katika soka ya Kenya, lala salama,”

Nahodha wa Kenya Michael Olunga pia aliwaongoza wenzake kuomboleza mauti ya Firat.

“Lala salama kocha,” akaandika Olunga kwenye X huku pia beki wa kushoto wa Stars Eric ‘Marcelo’ Ouma pia akiandika hivyo hivyo tu.

Jana, Shirikisho la Soka Nchini (FKF) lilituma taarifa ya kumwomboleza Firat.

Gor Mahia, Shabana na wanahabari pia walimwomboleza Firat na kumrejelea kama kocha aliyekuza soka ya Kenya kimataifa.

“Firat alifanya wachezaji wetu wajiamini na kuwa na uzoefu wa kucheza soka kimataifa. Mchango wake hautasahaulika na natuma rambirambi zangu kwa familia yake, marafiki na umma wa soka,” akaandika Mlezi wa Gor Mahia Eliud Owalo ambaye ni Waziri wa zamani wa Mawasiliano.

“Sisi ni wake Mungu na kwake tutarejea. Pumizka kwa Amani Engin Firat,” ikaandika Shabana katika ukurasa wao wa kijamii.