Sina hamu na wanaume kabisa, nimegundua wengi ni ‘wachezaji’, nishauri
SHIKAMOO shangazi. Nina umri wa miaka 30 na kwa sasa sina haja kabisa na wanaume. Hii ni kwa sababu wanaume wamenitenda. Kuna wakati tulipendana na mwanaume mwingine na akanicheza. Aliahidi kunioa ila baadaye akaruka. Kwa sasa napata shinikizo ya kuolewa kutoka kwa wazazi lakini mimi sitaki kuolewa. Nifanyeje?
Unafaa kutambua kuwa hisia zako ni halali. Kutendewa vibaya na wanaume kunaweza kuacha chuki ndani yako, na si lazima ujihusishe na ndoa ikiwa bado hauko tayari. Chukua nafasi hiyo kama fursa ya kujijua, kujithamini, na kuzingatia maisha yako bila shinikizo. Wakati utakapokuwa tayari, uamuzi wa ndoa utakuwa wa kweli, si wa kulazimishwa.
Mke wangu amebadilika kabisa tangu nipoteze kazi, hatusemezani tena!
Shikamoo shangazi. Nilifutwa kazi mwaka jana. Hali hii imetuathiri sana kifedha kama familia. Tangu wakati huo, mke wangu amebadilika sana huku kila mara akiteta kuwa nimemwachia majukumu yote. Hili linanishangaza kwani wakati nilikuwa na kazi nilikuwa nikifanya kila kitu. Tumezungumza na nimemueleza kuwa mambo yatakuwa sawa hivi karibuni ila ni kama napigia mbuzi gitaa. Kwa sasa hatuzungumzi kabisa. Je, hii ni kawaida?
Ni kawaida kwa watu kubadili tabia wakati changamoto za kifedha zinapoingia. Hata hivyo, ni muhimu kuwa na mazungumzo ya kweli. Jaribu kuzungumza naye umweleze jinsi unavyohisi na mume na mipango ya pamoja kuhusu jinsi ya kugawana majukumu hadi pale hali ya kifedha itakapoimarika. Kumbuka, mawasiliano na kuelewana huimarisha ndoa hata wakati wa changamoto.
Mume wangu asema sipendi familia yake!
Hujambo dada shangazi. Mume wangu anataka tuwajengee wazazi wake nyumba ilhali tuna majukumu mengine kama familia. Suala hilo limefanya tukosane sana. Najaribu kumueleza kuwa majukumu yetu kama familia ni ya maana sana kuliko kujenga nyumba. Anasema kuwa mimi siwapendi wazazi wake. Nitafanyaje ili aelewe kuwa mimi sina nia mbaya?
Kwanza tambua kuwa mapenzi yako kwa familia yako hayapunguzi heshima kwa wazazi wake. Jaribu kuzungumza naye kwa utulivu, umweleze kuwa huna nia mbaya bali unajali ustawi wa familia yenu. Toa mifano ya jinsi majukumu ya sasa yanavyohitaji muda na rasilimali zenu ili familia iendelee isonge mbele. Hili ni suala la kuelewana, si vita.
Anatumia pesa za biashara anavyotaka
Hujambo shangazi. Tulianzisha biashara na mume wangu ili kujiinua kimapato kama familia. Hata hivyo mambo yamebadilika sasa. Anajifanya kana kwamba biashara ni yake na anatumia faida kutoka kwa biashara bila kunishirikisha. Nikimuuliza anasema kuwa yeye ndiye simba wa nyumba na ana uhuru wa kufanya anachotaka. Je, hii ni haki?
Biashara ya ndoa au familia haiwezi kuwa mali ya mtu binafsi. Ikiwa mlianzisha pamoja, basi mnafaa kufanya maamuzi pamoja. Tabia ya mume wako kuishi kwa kauli kwamba yeye ndiye “simba wa nyumba” na kuendesha kila kitu peke yake si haki wala heshima ya ndoa. Iwapo hataki kukuelewa basi tafuta ushauri wa kisheria au wa ndoa ili kuhakikisha haki zako zinaheshimiwa.