Vizuizi vya polisi vyalemaza usafiri Nairobi wakati wa maadhimisho ya maandamano ya Gen Z Juni 25
Jiji la Nairobi limetengwana maeneo mengine ya nchi baada ya polisi kuweka vizuizi katika barabara kuu zote zinazoelekea jijini, hali iliyosababisha msongamano mkubwa wa magari na kuvuruga shughuli za usafiri kabla ya maandamano ya kuadhimisha mwaka wa pili tangu maandamano ya kupinga serikali ya Juni 25, 2025.
Maelfu ya wasafiri walikwama kwa saa kadhaa baada ya maafisa wa usalama kuzuia magari ya uchukuzi wa umma na kuwakagua madereva wa magari ya kibinafsi katika maeneo mbalimbali ya kuingia Nairobi.
Katika Barabara ya Thika, polisi waliweka vizuizi Ruiru, Githurai, Allsops na Kimbo, hatua iliyozuia matatu na mabasi kufika katikati mwa jiji.
Huko Kimbo, mamia ya abiria walikwama baada ya magari ya umma na ya kibinafsi yaliyokuwa yakielekea Nairobi kuzuiwa kuendelea na safari.
Hali kama hiyo ilishuhudiwa katika Barabara ya Mombasa ambako madereva waliokuwa wakitoka Machakos na Mombasa walitatizika kutokana na vizuizi kadhaa vya polisi.
Kizuizi kilichowekwa Mlolongo kuanzia saa kumi alfajiri kilisababisha msongamano mkubwa wa magari ulioenea kwa kilomita kadhaa. Hiki kilikuwa kizuizi cha tatu kwa magari yaliyokuwa yakitoka Machakos kuelekea Nairobi, huku vizuizi vingine vikiwa Kenya Israel na Kyumbi.
Msongamano huo ulifika hadi Lukenya, na kuwaacha madereva na abiria wakikwama kwa saa nyingi katika mojawapo ya barabara zenye shughuli nyingi nchini.
Polisi pia waliweka vizuizi Kangemi kwenye Barabara ya Waiyaki, ambapo mabasi na matatu yaliyokuwa yakijaribu kuingia jijini yalizuiwa. Ni magari machache tu yaliyokuwa yakiruhusiwa kuendelea baada ya ukaguzi mkali.
Magari yaliyokuwa yakitoka Nairobi hayakukumbwa na masharti hayo.
Kuingia katikati mwa jiji kulikuwa vigumu baada ya polisi kufunga barabara katika mizunguko ya Bunyala Road, City Stadium na Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta.
Katika mzunguko wa City Stadium, matatu na magari mengi kutoka maeneo ya mashariki mwa Nairobi yalizuiwa kuelekea kati kati ya jiji, hali iliyowalazimu mamia ya wakazi kutembea umbali mrefu.
Magari ya uchukuzi wa umma pia hayakuruhusiwa kupita mzunguko wa Hospitali ya Kenyatta, jambo lililokatiza kabisa huduma za usafiri kuelekea katikati mwa jiji.
Hatua hizo zilisababisha shughuli za biashara kuyumba huku wafanyakazi wengi wakishindwa kufika kazini kwa wakati na wafanyabiashara kukosa kufungua maduka yao.
Katika eneo la katikati mwa jiji, baadhi ya wafanyabiashara waliwaajiri walinzi wa kujitolea waliokuwa na marungu na kuvaa jezi za kuakisi mwanga ili kulinda biashara zao dhidi ya uporaji au uharibifu.
Hatua hizo kali za usalama zilijiri huku kukiwa na hofu ya vurugu wakati wa maandamano yaliyoandaliwa na vijana wa Gen Z kuwakumbuka waliouawa katika maandamano ya mwaka jana.
Maafisa wa usalama wako kwa wingi karibu na Bunge, Ikulu, ofisi za serikali na maeneo mengine muhimu.