Habari za Kitaifa

Afisi ya mke wa Kindiki yafyonza Sh45 milioni kwa miezi sita

Na DAVID MWERE March 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MDHIBITI wa Bajeti (CoB) Margaret Nyakang’o ameibua wasiwasi kuhusu matumizi ya Sh44.52 milioni na Afisi ya Mke wa Naibu Rais katika kipindi cha miezi sita ya kwanza ya mwaka wa kifedha wa 2025/26, licha ya afisi hiyo kutotengewa fedha zozote na Bunge la Kitaifa.

Afisi hiyo inashikiliwa na Dkt Joyce Njagi, ambaye ni mke wa Naibu Rais Prof Kithure Kindiki.

Kwa mujibu wa ripoti ya Mdhibiti wa Bajeti kuhusu utekelezaji wa bajeti ya serikali ya kitaifa kati ya Julai 1, 2025 na Desemba 31, 2025, afisi hiyo ilitumia fedha hizo licha ya kutokuwa na mgao rasmi wa bajeti. Ripoti hiyo kwa sasa imewasilishwa bungeni kwa uchunguzi zaidi.

Ripoti hiyo inaonyesha kuwa huenda shughuli za afisi hiyo zilifadhiliwa kupitia Afisi ya Naibu Rais, ambayo ilitengewa Sh3.07 bilioni katika mwaka wa kifedha wa sasa ikilinganishwa na Sh3.22 bilioni zilizotengewa afisi hiyo katika mwaka wa kifedha wa 2024/25.

“Afisi ya Mke wa Naibu Rais haikutengewa bajeti katika kipindi kilichokaguliwa, lakini ilirekodi matumizi ya Sh44.52 milioni,” alisema Dkt Nyakang’o katika ripoti hiyo.

Kwa kawaida, Afisi ya Naibu Rais ina jukumu la kuratibu na kusimamia utekelezaji wa sera, mipango na miradi ya serikali. Hata hivyo, kuwezesha shughuli za Afisi ya Mke wa Naibu Rais si mojawapo ya majukumu yaliyoainishwa chini ya afisi hiyo.

Mwaka wa 2024, Rais William Ruto aliamuru kufutiliwa mbali kwa bajeti za Afisi ya Mama wa Taifa pamoja na zile za wake wa Naibu Rais na Mkuu wa Mawaziri. Hatua hiyo ilichukuliwa kama sehemu ya juhudi za serikali kupunguza matumizi.

Uamuzi huo ulifuatia hatua ya Rais Ruto kukataa kutia saini Mswada wa Fedha wa mwaka 2024, uliopendekeza mikakati ya kukusanya Sh346 bilioni za ziada kupitia ushuru ili kufadhili bajeti ya mwaka wa kifedha wa 2024/25.

Mswada huo ulipingwa vikali na vijana wa kizazi cha Gen Z.

Wakati huo huo, serikali pia ilipunguza kwa asilimia 50 bajeti za siri katika baadhi ya afisi za serikali na kupendekeza kuunganishwa kwa mashirika 47 ya umma ili kupunguza matumizi.

Kabla ya hatua hiyo, jumla ya Sh1.3 bilioni zilikuwa zimetengwa kwa afisi tatu ambazo hazijawekwa wazi katika sheria za Kenya.

Kati ya fedha hizo, Afisi ya Mama wa Taifa ilikuwa imetengewa Sh696.6 milioni huku Afisi ya Mke wa Naibu Rais ikitengewa Sh557.6 milioni.

Kufutiliwa mbali kwa mgao huo wa fedha kuliacha baadhi ya mipango iliyoanzishwa na afisi hizo bila ufadhili rasmi wa serikali. Miongoni mwa mipango hiyo ni ule wa kuwawezesha wavulana.

Licha ya kusimamishwa kwa ufadhili huo, baadhi ya maafisa wa serikali waliomba Bunge la Kitaifa kurejesha angalau sehemu ya fedha hizo ili kulipa mishahara ya wafanyakazi wanaofanya kazi katika Afisi ya Mama wa Taifa.

Hata hivyo, ripoti ya Mdhibiti wa Bajeti inaonyesha kuwa matumizi ya fedha katika Afisi ya Naibu Rais yalikuwa tofauti kulingana na programu na vitengo mbalimbali.

Kwa mfano, mpango mdogo wa uratibu na usimamizi ulitumia bajeti yake yote, ukifikia kiwango cha matumizi cha asilimia 100.

Vilevile, shughuli zote za ndani na nje ya nchi zinazomhusisha Naibu Rais ziliratibiwa kikamilifu na kufikia asilimia 100.

Hata hivyo, mikutano ya mashauriano kati ya wizara, idara na mashirika ya serikali kuhusu uimarishaji wa mfumo wa thamani wa kahawa haikuonyesha matokeo yoyote katika miezi sita ya kwanza ya mwaka wa kifedha wa 2025/26.