Umemsaliti marehemu kakako Raila, Sifuna amwambia Oburu
VIONGOZI wa vuguvugu la Linda Mwananchi wameendelea kushambulia makubaliano kati ya chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA) na Orange Democratic Movement (ODM), wakisema kinara wa sasa wa chama chao, Dkt Oburu Oginga amesaliti kaka yake marehemu Raila Odinga.
Wakizungumza jijini Nairobi jana, viongozi hao walisema Serikali Jumuishi inayoongozwa na Rais William Ruto pamoja na Dkt Oginga imeshindwa kutekeleza misingi ya makubaliano yaliyozaa utawala huo.
Viongozi hao walikosoa uongozi wa ODM wakisema umesaliti ndoto na ajenda ya Raila kwa kushirikiana na serikali ambayo, kwa mujibu wao, haijatekeleza ajenda ya vipengele 10 hata baada ya mwaka mmoja.
Katika ripoti yao iliyopewa jina “Ajenda Kumi na Uongo”, walikosoa kila kipengele cha ajenda hiyo, wakionyesha kile walichodai kuwa ni kutotekelezwa kwa makubaliano kati ya chama tawala cha UDA na ODM.
Katika tathmini yao kuhusu utekelezaji wa ajenda hiyo, walisema matokeo yake yamekuwa duni sana, wakitoa alama ya moja kati ya kumi.
Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna alisema tangu mwanzo kamati hiyo ilitakiwa kutoa ripoti ya maendeleo kila baada ya miezi miwili na kuwasilisha ripoti ya mwisho ifikapo Machi 7, 2026.
Bw Sifuna alisema kilichoshuhudiwa katika mkutano uliofanyika katika Jumba la Kimataifa la Mikutano (KICC) Jumanne, ni “tamthilia ya aibu” iliyolenga kuwafanya Wakenya waamini kuwa makubaliano hayo yalitekelezwa kikamilifu.
“Kilichotokea jana kilikuwa maigizo ya kuwadanganya wananchi kwamba makubaliano ya ushirikiano yametekelezwa ilhali ukweli ni kwamba hakuna kilichofanyika,” alisema Sifuna.
Sifuna pia alikosoa hatua ya Rais William Ruto kudai kuongeza muda wa kamati hiyo kwa siku 60 zaidi, akisema uamuzi huo hauna msingi wa kisheria.
Alisema kulikuwa na mkanganyiko katika mkutano huo baada ya baadhi ya viongozi kudai kuwa makubaliano hayo hayakuwa na muda maalum wa utekelezaji.
“Mkanganyiko ulioshuhudiwa katika mkutano wa KICC ni ushahidi kwamba wanaohusika wanajua wanawadanganya Wakenya na hata kujidanganya wenyewe,” alisema.
Alisema kundi la Wabunge wa ODM halina mamlaka kikatiba ya kufanya maamuzi kama yale yaliyotangazwa katika mkutano huo.
Alisema uamuzi wa kuongeza muda wa makubaliano hayo ni kinyume cha katiba ya chama na hivyo ni batili.
Aliongeza kwamba iwapo makubaliano hayo yangekuwa yametekelezwa, Wakenya wangeona mabadiliko kwa macho yao.
Alitaja visa vya utekaji nyara na mauaji ya kiholela vinavyodaiwa kufanywa na vyombo vya usalama akisema kama vingekuwa vimekoma baada ya kutiwa saini kwa makubaliano hayo, wananchi wangejua.
Kadhalika alisema kama kaunti zingepokea Sh450 bilioni za mapato ya mgao katika mwaka wa kifedha wa sasa, jambo hilo lingekuwa wazi kwa kila mtu.
“Pia, kama serikali ya Rais Ruto ingeheshimu uhuru na vyama vya kisiasa kama ilivyoahidi, hilo lingeonekana wazi,” alisema.
“Nia ya Raila Odinga ilikuwa kuhakikisha kwamba kila jukumu lililotengwa kama la ugatuzi linatekelezwe na serikali za kaunti. Badala ya kuheshimu urithi wa Baba, ambaye alijulikana kama baba wa ugatuzi, serikali ya kitaifa sasa inanyakua majukumu ambayo yanapaswa kutekelezwa na serikali za kaunti,” alisema.
Gavana wa Siaya James Orengo alisema ajenda ya vipengele kumi ilikuwa tu makubaliano ya muda ya kutuliza hasira za wananchi wakati wa maandamano ya vijana mwaka 2024.
Bw Orengo alisema hati hiyo ilikuwa kama “makubaliano ya kusitisha mapambano” ili kuwashawishi Wakenya watulie kidogo serikali ikiahidi kutekeleza mageuzi.
Lakini alisema muda wa makubaliano hayo sasa umeisha bila utekelezaji wowote.
Orengo alisema ni wakati wa Wakenya kuanza kudai mabadiliko badala ya kusubiri hadi uchaguzi wa 2027.
“Sasa ndio wakati wa kuanza mchakato wa kuleta mabadiliko nchini. Hili halitafanywa na Bunge wala taasisi nyingine ambazo zimepunguzwa nguvu. Mabadiliko yatatoka kwa wananchi wenyewe,” alisema.