Unyama: Mwanamke auawa kikatili damu ikikusanywa kwenye ndoo
FAMILIA ya mwanamke mmoja Kaunti ya Murang’a ina majonzi baada ya mwili wake kupatikana ndani ya chumba kidogo kijijini huku damu yake ikiwa imekusanywa ndani ya ndoo.
Mwili wa Mercy Wamaitha, mwenye umri wa miaka 44, kutoka kijiji cha Kiamakumi eneo bunge la Maragua ulipatikana Machi 8, 2026 ndani ya chumba cha udongo katika hali ya kutisha kiasi kwamba majirani walihusisha tukio hilo na shughuli za dhehebu la siri.
Hata maafisa wa Uchunguzi wa Jinai (DCI) eneo la Murang’a Kusini walionekana kushtushwa na walichokiona, kiasi kwamba mashahidi walisema waliondoka wakiacha ndoo iliyokuwa na damu.
Ilibidi Naibu Kamishna wa Murang’a Kusini Bernard Odinoh kuwapigia simu ya dharura ili kuwaamuru maafisa hao warudi eneo la tukio kuondoa damu hiyo ambayo tayari ilikuwa imeanza kuoza baada ya siku nne.
Kulingana na ripoti ya awali ya uchunguzi iliyotolewa na kamanda wa polisi wa Murang’a Kemboi Kimaiyo, mwanamke huyo huenda aliuawa kutokana na mgogoro wa kimapenzi unaohusisha watu watatu.
Ripoti inaeleza kuwa Wamaitha alikuwa mkazi wa kijiji cha Iganjo katika wadi ya Kamahuha na aliacha shule akiwa Darasa la Tano ili kuolewa katika kijiji cha Kianjiru-ini, umbali wa takriban kilomita 25.
Alikuwa ameolewa na mwanamume anayetambulika kama Macharia wa Njeri, na walibarikiwa na watoto sita wenye umri wa kati ya miaka mitano na 25. Hata hivyo, katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita ndoa yao ilikumbwa na migogoro na Wamaitha aliondoka nyumbani mara kadhaa.
Baadaye alianza kutafuta kazi za nyumbani katika miji mbalimbali, na ndipo inadaiwa alianza uhusiano wa kimapenzi na mwanamume mwingine. Mwili wake ulipatikana katika nyumba ya Justus Kamau, ambaye sasa ni mshukiwa na tayari amefikishwa mahakamani huku polisi wakiomba muda zaidi kukamilisha uchunguzi.
Mumewe Macharia alisema alishtuka sana kusikia habari za kifo chake. “Kwa miaka mitatu iliyopita nimekuwa nikimrudisha nyumbani mara kadhaa kutoka nyumba hiyo. Aliondoka nyumbani siku tatu kabla ya kifo chake na nilikuwa napanga kumfuata. Inaniuma sana, bado nampenda,” alisema.
Ripoti ya polisi inaonyesha kuwa Wamaitha alikuwa akitembelea nyumba hiyo mara kwa mara. Katika ziara yake ya mwisho, alikuwa ameishi hapo kwa siku tatu tu. Inadaiwa kuwa wawili hao walikuwa wakitafuta vibarua mchana, kulipwa jioni kisha kwenda kunywa pombe katika kituo cha biashara kilicho karibu kabla ya kurudi chumbani usiku.
Usiku wa Machi 7, nyanya ya mshukiwa mwenye miaka 75 Beatrice Wangui alisema wawili hao walichukua sahani ya ugali na maharagwe kutoka jikoni kwake.
Alisema aliamshwa na kelele majira ya saa nane usiku. Alipotoka nje, alikuta majirani kadhaa pamoja na Diwani wa Ichagaki, Hillary Muigai, wakiwa wamekusanyika.
Polisi walipofika eneo hilo walikuta kitanda kilichochafuka, chakula ambacho hakikuwa kimeguswa, pamoja na ndoo iliyokuwa na damu. Pia kulikuwa na damu sakafuni na kisu kilichokuwa na damu.
Ripoti ya uchunguzi wa maiti iliyofanywa Machi 12 ilionyesha Wamaitha alikuwa na majeraha matano ya kudungwa kwa kisu — manne katika paja la kulia na moja katika kiganja cha mkono wa kulia. Majeraha hayo yalipasua mshipa mkubwa wa damu wa paja na akapoteza damu kwa wingi kusababisha kifo chake.
Kamanda wa polisi wa Murang’a Kusini Charity Karimi alisema Kamau alikamatwa na mahakama imeruhusu azuiliwe hadi Aprili 2, 2026 uchunguzi ukiendelea.
Baba ya marehemu, Joseph Mwaniki Njuguna, alisema anachotaka ni haki itendeke kwa binti yake. Aliongeza kuwa ingawa Wamaitha alikuwa na watoto sita, hakuna mwanaume aliyewahi kufika nyumbani kwake kujitambulisha rasmi kama mume wake.