Siasa

Sifuna afaulu kukinga jina ‘Linda Mwananchi’ dhidi ya kutwaliwa

Na JUSTUS OCHIENG March 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

OFISI ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa imekataa ombi la kuhifadhi jina Linda Mwananchi Party of Kenya, hatua ambayo ni ushindi kwa vinara wa vuguvugu la Linda Mwananchi.

Hatua hiyo pia inazima mzozo wa kisiasa uliokuwa umeibuka kuhusu matumizi ya kaulimbiu hiyo.

Katika barua rasmi kwa mwombaji, Msajili wa Vyama vya Kisiasa John Cox Lorionokou, alimjulisha Charles Wanyonyi kwamba jina lililopendekezwa haliwezi kuidhinishwa kisheria kwa sababu linafanana na kaulimbiu nyingine na pia linaibua masuala ya maslahi ya umma.

“Kuhusiana na ombi lako la kuhifadhi jina lifuatalo: Linda Mwananchi Party of Kenya (LMPK), ombi lako limezingatiwa kwa mujibu wa sheria lakini jina hilo limekataliwa kwa kuwa linafanana na kaulimbiu nyingine iliyokwisha kuhifadhiwa—Linda Mkenya, Boresha Kenya—na pia kwa kuzingatia maslahi ya umma, hivyo kukiuka Kifungu cha 8 cha Sheria ya Vyama vya Kisiasa,” aliandika Bw Lorionokou akimshauri mwombaji kuwasilisha majina mengine kwa ukaguzi.

Uamuzi huo unasitisha kwa sasa mipango ya kusajili chama hicho kipya na pia kuhitimisha kwa muda mvutano uliokuwa umeibuka kati ya Bw Wanyonyi na kundi la wanasiasa wa upinzani waliopinga ombi lake.

Kukataliwa kwa jina hilo kunajiri baada ya majuma kadhaa ya mvutano kuhusu umiliki wa kauli “Linda Mwananchi”, ambayo imekuwa ikihusishwa na mikutano ya hadhara iliyoandaliwa na kundi la wanasiasa wanaomuunga mkono Katibu Mkuu wa Orange Democratic Movement (ODM) Edwin Sifuna.

Mzozo huo ulianza baada ya Bw Wanyonyi kuwasilisha ombi la kuhifadhi jina Linda Mwananchi Party of Kenya, jambo lililosababisha pingamizi la haraka kutoka kwa kundi la Bw Sifuna. Kundi hilo lilidai kuwa kaulimbiu hiyo tayari imekuwa ishara ya kampeni yao ya kuhamasisha raia.

Pingamizi hilo liliwasilishwa kupitia kampuni ya mawakili ya Henia Anzala and Associates kwa niaba ya baadhi ya wanasiasa wanaomuunga mkono Bw Sifuna.

Miongoni mwa waliounga mkono pingamizi hilo ni Bw Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na mwenzake wa Saboti Caleb Amisi miongoni mwa wengine.

Katika barua yao ya pingamizi kwa Msajili wa Vyama vya Kisiasa, viongozi hao walisema kauli “Linda Mwananchi” imekuwa ikihusishwa kwa karibu na ujumbe wao wa kisiasa.

Walieleza kuwa kaulimbiu hiyo imetumika katika mikutano yao kote nchini na sasa imegeuka kuwa jukwaa la kampeni ya mageuzi inayolenga kupinga kile wanachotaja kuwa utawala mbovu serikalini.

Kwa mujibu wao, kuruhusu mtu binafsi kusajili chama cha kisiasa kwa kutumia kaulimbiu hiyo bila ushiriki wao kunaweza kupotosha umma.

Pia, walionya kuwa hatua kama hiyo inaweza kufungua mlango kwa watu kujinufaisha kisiasa kwa kutumia umaarufu wa vuguvugu lao kukusanya fedha au kuvutia wafuasi kwa misingi ya udanganyifu.

“Kutokana na hayo, wateja wetu wanaomba ofisi yako kuzuia jaribio hilo la kuwalaghai Wakenya kupitia ujanja wa kisiasa kwa kukataa ombi hilo,” mawakili hao waliandika katika pingamizi lao.

Kabla ya uamuzi wa msajili kutolewa, Bw Wanyonyi alikuwa amepinga vikali madai hayo na kuashiria uwezekano wa mvutano wa kisheria.

Kupitia mawakili wake, kampuni ya Wanzau, Odhiambo and Associates Advocates, alisema pingamizi la kundi la Bw Sifuna halikuwa na msingi wowote wa kisheria chini ya Sheria ya Vyama vya Kisiasa.

Katika majibu yaliyowasilishwa kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa, mawakili hao walisisitiza kuwa mteja wao alitumia haki yake ya kikatiba kama raia wa Kenya kuwasilisha ombi la kusajili chama cha kisiasa.

Walifafanua pia kuwa Bw Wanyonyi hakuwa akifanya hivyo kwa niaba ya kiongozi yeyote wa kisiasa.

“Tunapenda kubainisha kuwa mteja wetu hahusiani na watu waliotajwa katika barua ya Henia Anzala and Associates,” waliandika.

“Mteja wetu aliwasilisha ombi hilo kama raia wa Kenya na kwa kutumia haki zake za kiraia na kisiasa zinazolindwa na Katiba.”

Mawakili hao pia walieleza kuwa kauli “Linda Mwananchi” haijawahi kusajiliwa na mtu au shirika lolote kama jina la chama cha kisiasa.

Mzozo huo ulijikita zaidi katika tafsiri ya Kifungu cha 8 cha Sheria ya Vyama vya Kisiasa kinachobainisha mazingira ambayo Msajili anaweza kukataa jina la chama cha kisiasa.

Chini ya sheria hiyo, Msajili anaweza kukataa ombi ikiwa jina lililopendekezwa ni chafu, linafanana na la chama au taasisi nyingine, limepigwa marufuku au linaonekana kwenda kinyume na maslahi ya umma.

Wakati huo huo, mjadala kuhusu jina hilo pia ulivutia kamati ya ulinzi ya Bunge la Kitaifa inayoongozwa na Mbunge wa Belgut Nelson Koech, ambaye alieleza wasiwasi kuhusu athari za kauli “Linda Mwananchi”.

Bw Koech alisema kauli hiyo inaweza kuchanganya majukumu ya kikatiba kuhusu usalama wa taifa.

Alibainisha kuwa jukumu la kulinda wananchi na kutetea nchi limekabidhiwa mashirika ya usalama ya serikali kama Huduma ya Polisi na Jeshi la Kenya.

Aidha alirejelea operesheni ya kijeshi Operation Linda Nchi, akisema matumizi ya lugha kama hiyo katika siasa yanaweza kwa bahati mbaya kuibua taswira za makundi ya kijeshi.

Ingawa hakuna ushahidi unaoonyesha chama kilichopendekezwa kinahusishwa na shughuli kama hizo, matamshi hayo yalionyesha uzito unaozunguka matumizi ya kauli hiyo.