Kampeni zachacha Ol Kalou zikibaki siku 10 kura zipigwe
HUKU zikisalia siku kumi pekee kabla ya uchaguzi mdogo wa ubunge wa Ol Kalou, ushindani huo umegeuka kuwa kipimo cha nguvu za kisiasa katika eneo la Mlima Kenya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.
Mirengo inayoshindana imetaja uchaguzi huo kama kura ya maamuzi kuhusu mwelekeo wa kisiasa wa eneo hilo, huku kila upande ukitaka kuthibitisha kuwa unaungwa mkono na wapigakura wengi.
Wagombeaji wanaopigiwa upatu ni Douglas Waweru wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP), Muchina Nyaga wa chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA) na Wilson Kigwa wa Jubilee.

Wengine sita pia wanawania kiti hicho.
Kiti hicho kilibaki wazi baada ya kifo cha Njuguna Kiaraho wa chama cha Jubilee mnamo Machi 29, 2026.
Mgombeaji wa Jubilee, Bw Kigwa, anakabiliwa na changamoto baada ya kiongozi wa chama hicho, rais mstaafu Uhuru Kenyatta, na mgombea wake wa urais Dkt Fred Matiang’i, kutoshiriki kampeni zake.
Aidha, Mbunge Mteule wa Jubilee Sabina Chege ameasi chama chake na sasa anamuunga mkono mgombeaji wa UDA.
Uchaguzi huo umegeuka kuwa pambano kati ya serikali ya Rais William Ruto na upinzani unaoongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.
Bw Gachagua ametangaza kuwa atafanya kampeni Ol Kalou kwa siku tatu kuanzia Julai 10 kabla ya kampeni kufungwa Julai 13.
Nyumba ya Seneta wa Nyandarua John Methu katika kijiji cha Mugumo imekuwa kituo cha mikutano ya kisiasa ya wafuasi wa Bw Gachagua, huku viongozi wa serikali wakifanya ziara mbalimbali za maendeleo wakiahidi miradi ili kuvutia wapigakura.
Kati ya wagombeaji tisa, ni Bw Nyaga pekee anayemuunga mkono waziwazi Rais Ruto na serikali ya UDA, huku wengine wakiwa upande wa upinzani.
Katika mdahalo uliopeperushwa na Inooro TV Julai 5, Bw Nyaga alikabiliwa na mashambulizi kutoka kwa wagombeaji wengine lakini alitetea sera zake.
Bw Gachagua amesema idadi kubwa ya wagombea ni ishara ya demokrasia na kwamba hakuna anayepaswa kuzuiwa kugombea.
Hata hivyo, wachambuzi wa siasa wanaonya kuwa Bw Gachagua ndiye anayehatarisha zaidi kisiasa iwapo mgombea anayemuunga mkono atashindwa, kwani hali hiyo itadhoofisha madai yake ya kuwa kinara wa kisiasa wa Mlima Kenya na kuathiri azma yake ya kuwania urais mwaka 2027.
Kwa upande mwingine, Naibu Rais Kithure Kindiki amesema ushindi wa UDA katika uchaguzi huo utathibitisha kuwa siasa za ubaguzi na kujitenga hazina nafasi katika eneo la Mlima Kenya.
Shinikizo pia linaongezeka kwa Prof Kindiki kushiriki moja kwa moja katika kampeni hizo, huku matokeo yakitarajiwa kuathiri nafasi yake ya kuendelea kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto mwaka 2027.
Mbunge wa Laikipia Mashariki Mwangi Kiunjuri, ambaye ni mmoja wa viongozi wanaompigia debe mgombea wa UDA, alisema chama hicho kina uhakika wa kushinda.
“Tunaendelea vizuri na takwimu zetu zinaonyesha tutashinda. mgombea wetu ndiye bora,” alisema.
Lakini Mbunge wa Kipipiri Wanjiku Muhia, anayemuunga mkono Bw Gachagua, alisema mgombea wa DCP ndiye anayeongoza.
Alisema uchaguzi huo unalenga kuthibitisha kuwa eneo la Mlima Kenya linaweza kufanya maamuzi yake ya kisiasa bila kushinikizwa.
Mchambuzi wa siasa Malila Munywoki amesema uchaguzi huo utakuwa mtihani muhimu kwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) na Idara za usalama kuonyesha vinaweza kusimamia uchaguzi huru, wa haki na wa amani kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Naye Gavana wa Nyandarua Kiarie Badilisha hajaweka wazi mgombeaji anayemuunga mkono, lakini amekuwa akiwaambia wakazi kuwa kisiasa yuko upande ambao wananchi wengi wa kaunti hiyo wanaunga mkono, kauli ambayo imezua uvumi kuwa huenda akahama chama kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.