Akili MaliMakala

Msukumo wa kidijitali kulinda mbegu

Na SAMMY WAWERU March 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MPANGO mpya wa kimataifa unaolenga kubadilisha jinsi mazao yanavyofuatiliwa, kulindwa na kutumika umezinduliwa, hatua inayotajwa kuwa muhimu katika kuimarisha usalama wa chakula siku zijazo wakati ambapo dunia inakabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Mradi huo unaojulikana kama Securing Our Seeds (SOS): Digital Innovation for Global Crop Diversity Conservation ulizinduliwa mwezi uliopita, Februari 2026 na Crop Trust.

Crop Trust ni shirika la kimataifa lisilo la kiserikali, linalolenga kuhifadhi na kuhakikisha upatikanaji wa mazao duniani ili kuimarisha usalama wa chakula.

Mpango huo umefadhiliwa kupitia ruzuku kutoka Google.org kupitia mpango wake wa Google.org AI Collaborative: Food Security, kwa thamani ya dola milioni mbili za Amerika (takriban Sh258 milioni).

Kulingana na Crop Trust, mradi huo unalenga kuboresha mfumo wa benki za mbegu za mazao duniani (seed bank) kwa kuimarisha usimamizi wa taarifa, kuongeza ujuzi wa kidijitali na kuhimiza matumizi ya teknolojia mpya kama vile Artificial Intelligence (AI).

Shirika hilo limejitolea kujenga na kusaidia mtandao wa kimataifa wa benki za vinasaba (gene banks) zinazohifadhi mazao tofauti ya kilimo.

Zaidi ya vituo 850 duniani vinahifadhi mamilioni ya sampuli za mbegu na mimea, ambazo kijumla ni muhimu katika kuzalisha mazao yanayostahimili joto kali, ukame, wadudu na magonjwa.

Mtaalamu kutoka Chuo Kikuu cha Egerton akielezea kuhusu mfumo wa mbegu asili. Picha|Sammy Waweru

Sampuli hizo, pia, husaidia kuboresha lishe na kuongeza kipato cha wakulima.

Hata hivyo, licha ya mafanikio hayo, maghala mengi ya mbegu yanakabiliwa na changamoto kubwa.

Mifumo dhaifu ya usimamizi wa taarifa na matumizi madogo ya data iliyopo, yamesababisha sehemu kubwa ya tofauti ya mazao yaliyohifadhiwa kutotumika ipasavyo au kuwa katika hatari ya kupotea.

“Utofauti wa mazao unapotea kimyakimya wakati ambapo dunia inauhitaji zaidi,” anasema Dkt Stefan Schmitz, Mkurugenzi wa Crop Trust.

“Kwa msaada wa Google.org, tunachukua hatua muhimu kulinda utofauti wa mazao, katika benki za vinasaba, mbegu na mashambani, ili kuimarisha usambazaji wa chakula kwa minajili ya siku zijazo,” anaoongeza.

Kupitia mradi wa Securing Our Seeds, Crop Trust itasaidia maghala kumi ya kitaifa ya vinasaba katika nchi za Kusini mwa dunia kuwa vituo mahiri vya data.

Hatua hiyo itaafikiwa kwa kupanua matumizi ya programu maalum ya usimamizi wa taarifa za benki za vinasaba inayojulikana kama GRIN-Global Community Edition, pamoja na kutoa mafunzo faafu ya usimamizi wa taarifa ili kuongeza ujuzi wa kidijitali.

Upatikanaji bora wa data unatarajiwa kusaidia watafiti, wazalishaji wa mbegu na wakulima kupata kwa urahisi taarifa kuhusu aina ya mazao inayofaa kwa mazingira yao na changamoto za tabianchi.

Kulingana na Dkt Schmitz, bila data inayopatikana kwa urahisi na inayoweza kuaminika, rasilimali muhimu za kinasaba hubaki kufichwa, jambo linalopunguza uwezo wake kusaidia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuimarisha usalama wa chakula duniani.

Pakiti zenye mbegu za mboga. Picha|Sammy Waweru

Mradi huo, pia, utachunguza namna AI inaweza kutumika kutambua na kufuatilia hatari zinazoandama mazao katika mashamba na mifumo ya ikolojia ya porini.

Kwa sasa, hakuna mfumo wa kimataifa unaofuatilia mahali ambapo bioanuwai (biodiversity) ya kilimo inapotea au unaoeleza sababu za upotevu huo.

Kama sehemu ya mradi wa Securing Our Seeds, Crop Trust itachunguza uwezekano wa kuunda mfumo wa tahadhari wa mapema unaotumia AI, utakaochanganya data mbalimbali ili kutambua na kuonyesha hatari kwa utofauti wa mazao kupitia ramani ya kimataifa ya kidijitali.

Mfumo huo unaweza kusaidia maghala ya mbegu na wanasheria kuchukua hatua za mapema kabla rasilimali muhimu za kinasaba hazijapotea kabisa.

“Hatua za mapema kwa kutumia AI zinaweza kusaidia uhifadhi wa mazao katika kiwango kipya kabisa. Ushirikiano huu unafungua sura mpya katika kuifanya sekta ya kilimo iende sambamba na mabadiliko ya tabianchi,” anasema Dkt Sarada Krishnan, Mkurugenzi wa Programu katika Crop Trust.

Wataalamu wa kilimo wanasema kuwa matumizi ya ‘akili bandia’ yanaweza kuwa na mchango mkubwa katika kupambana na uhaba wa chakula kwa kuboresha hifadhi ya mazao, utafiti wa kuzalisha mbegu bora na maamuzi ya kisera.

Kupitia mradi wa SOS, Crop Trust na Google.org, wanalenga kujenga mfumo imara wa kimataifa wa benki za vinasaba na mbegu uliounganishwa kidijitali, ili kuhakikisha utofauti wa mazao umehifadhiwa, umeandikwa vizuri na unatumika ipasavyo kwa vizazi vijavyo.