Kundi la wanawake linavyopata faida kwa kukausha mboga za kienyeji kuwahi soko la nje
KATIKA eneo la Lari, Kaunti ya Kiambu — linalojulikana sana kwa uzalishaji wa mboga za kisasa na za kienyeji, mageuzi tulivu yanaendelezwa katika sekta ya mboga.
Kikundi cha Cheer Up Program, kilichoanzishwa mwaka 2003 kama Shirika la Kijamii (CBO) kusaidia watu wasiojiweza, sasa kinabadilisha maisha ya wakazi wengi wanaotegemea kilimo cha mboga.
Kundi hilo la wanachama 20 limegundua fursa yenye faida kwa kukausha mboga za kienyeji kama vile managu (sucha), terere, saga na kunde, pamoja na mboga zingine na za kisasa kama sukuma wiki, spinachi na kabichi.
Bidhaa zao sasa zinauzwa masoko ya nje ya Kenya.
Kwenye kituo chao kilichopo kijiji cha Matathia, Lari, pia hukausha mboga asilia aina ya thafai, mimea asilia kama rosemary, pamoja na matunda aina ya mananasi na ndizi mbichi.
Aidha, ndizi husagwa kuwa unga kwa kutumia mashine ya kusaga nafaka na kuchanganywa na terere, thafai na muhogo kutengeneza unga wa uji wenye lishe na virutubisho bora, hasa kwa watoto.

Meneja wa Mikakati, Martin Chege, anasema karibu asilimia 30 ya mboga wanazokausha huuzwa katika soko la kimataifa.
“Kwa sasa Cheer Up husambaza mboga zilizokaushwa katika nchi za Uarabuni za Mashariki ya Kati (Middle East), Amerika, Canada na baadhi ya nchi za bara Uropa,” Chege anaelezea.
Nchini Kenya, bidhaa hizo pia huuzwa katika maeneo kame na nusu kame (ASAL) haswa wakati wa kiangazi na ukame.
Kulingana na Tabitha Muthoni, Meneja mwingine wa Mikakati anayehusika na utafutaji na ukusanyaji wa mboga na mafunzo kwa wakulima, kiwanda cha Cheer Up Program kimekua ambapo uzalishaji umeongezeka kutoka kukausha kilo 500 kwa siku hadi maelfu.
“Kila aina ya mboga hukausha takriban tani moja kila baada ya siku tatu, isipokuwa kabichi ambazo hufikia tani 1.5,” Muthoni anasema.
Bei hutegemea aina ya mboga. Kilo moja ya sukuma wiki au spinachi zilizokaushwa huuzwa Sh700, huku mboga za kienyeji huanzia Sh800 kwa kilo.
Mbali na wanachama wa kikundi, Cheer Up Program imetia saini mikataba na wakulima zaidi ya 40 kutoka maeneo ya Ndeiya, Kijabe na Githunguri, yote yakiwa ndani ya Kaunti ya Kiambu.
“Wanapotusambazia mboga huwalipa Sh50 kwa kilo,” Muthoni akaambia Akilimali Dijitali kwenye mahojiano ya kipekee.
Hata hivyo, mboga hizo lazima ziafiki viwango vya ubora kupitia vigezo walivyoweka kama kundi la uchakataji.
Chege anasisitiza kuwa mboga lazima zilimwe kwa njia ya kiasili – bila kutumia kemikali ili zihifadhi uhalisia wake wa kiasilia.

“Baada ya kuvunwa, hupangwa, kuoshwa, kutumbukizwa kwenye maji ya chumvi yanayochemka kwa dakika chache, kisha kupozwa kabla ya kupelekwa kwenye kikaushio cha kisasa cha kawi ya jua (sola),” Chege anafafanua.
Kulingana na Monicah Wacuka, mkulima na mmoja wa waanzilishi, wazo la kukausha mboga lilianza mwaka 2007.
“Tulianza kama kikundi cha kanisa kilicholenga kusaidia yatima wanaosoma shuleni,” anasema.
Baadaye, kilipanua huduma zake na kuanza kuchakata mboga lengo likiwa kusaidia wanachama na wakulima.
Kwa miaka mingi, kikundi hicho kimepiga hatua kubwa. Mwaka 2024 waliboresha vifaa vya huduma ambapo kilikumbatia kikaushio cha kisasa cha jua kinachotumia pia makaa maalum wakati wa baridi au mvua.
Leo hii, mradi huo umeajiri wafanyakazi watano wa kudumu na umesaidia familia nyingi kujipa mapato.
Mwanachama Rose Wangui, mama wa watoto watatu, anasema; “Mapato hayo yameniwezesha kusomesha watoto wangu.”
Ingawa bado wanakabiliwa na changamoto kama vile ukosefu wa mikopo na miundombinu duni ya barabara, wanachama wa Cheer Up Program wanaamini ushirikiano wao ndio nguvu kubwa ya mafanikio waliyoandikisha.
“Safari ya ujasiriamali imetufundisha umuhimu wa maarifa, utafiti wa masoko na kuwa na malengo makuu,” Monicah Wacuka anasema.