Joto lapanda Emurua Dikirr mjane wa Ng’eno akitangaza azma
JOTO la kisiasa limeanza kupanda eneobunge la Emurua Dikirr wiki moja tu baada ya Mbunge wa eneo hilo Johana Ng’eno kuzikwa.
Bw Ngéno na watu wengine watano waliaga dunia kwenye ajali ya helikopta katika eneo la Nandi.
Makundi matatu yanayopigania kiti hicho yamechipuka baada ya Mjane wa Ng’eno, Naiyanoi Ng’eno kutajwa na wanafamilia na uko kama mrithi wa mumewe eneobunge la Emurua Dikirr.
Hata hivyo, baadhi ya watu wa ukoo wa Kapkoan anakotoka marehemu Ng’eno walimuidhinisha Benard Rono ambaye anafanya kazi na Serikali ya Kaunti ya Narok kama mwaniaji wanayempendelea.
Bw Keter amewania kiti hicho mara mbili akipoteza kwa Ng’eno katika chaguzi mbili zilizopita.
Wakati wa mazishi ya Ng’eno, Mama Mary Temas, mamake marehemu mbunge huyo aliwaomba Rais William Ruto na Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki wakubali mrithi wa Bw Ng’eno atoke katika familia hiyo.
Nayianoi, ambaye ni wakili ni limbukeni kwenye siasa na hajakuwa akijihusisha sana na masuala ya siasa tangu aolewe na Bw Ng’eno mnamo 2018 akiwa na umri wa miaka 22.
“Nashukuru sana kutokana na uamuzi wa familia, ukoo na wakazi wa eneobunge hili kwa sababu nalenga kuendeleza ndoto na maono ya marehemu mume wangu. Nawaomba wakazi wa eneobunge hili waniunge mkono uchaguzi mdogo ukiwadia na sote tushiriki kampeni za amani,” akasema Bi Naiyanoi.
Hata hivyo, italazimu mjane huyo apitie mchujo wa UDA na inakisiwa tangazo la familia la kumuidhinisha lililenga kuzuia mgawanyiko wa ndani kwa ndani.
“Tunawaomba wakazi wamruhusu Nayianoi akamilishe muhula wa mumewe kisha katika uchaguzi mkuu ujao uamuzi utafanywa kuhusu mwelekeo wa kufuatwa,” akasema David Ngetich ambaye ni mmoja wa watu wa ukoo wa Kapkoan.
Kulingana na sajili ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC), Emurua Dikirr ina wapigakura 44,477.
Ina wadi za Ilkerin, Mogondo, Kapsasian na Ololmasani ambazo zinakaliwa sana na jamii ya Kipsigis.