Habari

Gavana ahimiza amani mrengo wa Linda Mwananchi ukijiandaa kutua Mombasa

Na KNA March 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

GAVANA wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir, ametoa wito wa utulivu na amani wakati wanasiasa wa mrengo wa Linda Mwananchi wanapopanga kuzuru kaunti hiyo punde baada ya Ramadhani.

Seneta wa Nairobi, Bw Edwin Sifuna, anayeongoza mrengo huo alithibitisha mpango wa kufanya mkutano wa hadhara katika uwanja wa Tononoka, huku akidai kuna pingamizi kutoka kwa wapinzani wao.

Hata hivyo, Bw Nassir akizungumza katika eneobunge la Changamwe alisema kila mtu anakaribishwa kufanya mkutano wa kisiasa Mombasa, lakini akasisitiza kuwa mikusanyiko hiyo lazima iwe ya amani na isiyo na vurugu, jinsi ilivyokuwa Kitengela na Kakamega awali.

“Hapa ni mahali pa amani. Waje, wazungumze na wananchi, na waondoke katika jiji letu kwa amani,” alisema Bw Nassir.

Wakati huo huo, alipuuza mvutano kati ya viongozi wa UDA na ODM Mombasa, akisisitiza Mkutano wa Kitaifa wa Wajumbe wa ODM (NDC) utafafanua mwelekeo kuhusu jinsi ya kushirikiana na UDA.

“Tutaamua jinsi tutakavyoshirikiana nao, muundo wake utakuwa upi, wao watafanya nini na sisi tutafanya nini. Kwa sasa ni nia tu, na baada ya NDC tutakubaliana kuhusu hatua za kuchukua,” akasema.