Kimataifa

Japan, Australia zakataa wito wa Trump kutuma meli za kivita Iran

Na REUTERS March 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TOKYO, Japan

WITO wa Rais wa Amerika Donald Trump kwa mataifa rafiki kusaidia kufungua Mkondo wa Hormuz kufanikisha usafirishaji wa mafuta ulikataliwa jana baada ya Japan na Australia kusema hazitatuma meli za kivita kusindikiza meli zinazosafirisha bidhaa hiyo kupitia mkondo huo.

Mnamo Jumapili, Trump aliyataka mataifa washirika wa Amerika yanayotegemea mafuta kutoka eneo hilo la Ghuba yaungane kuimarisha usalama katika mkondo huo ambako asilimia 20 ya mafuta yote duniani hupitishiwa.

“Nataka mataifa haya kuingilia kati na kulinda ngome yao kwa sababu ni ngome yao. Ni mahala ambako wanapata kawi ya mafuta wanayotumia,” Trump aliwaambia wanahabari akiwa ndani ya ndege yake rasmi, “Air Force One” akiwa njiani kutoka Florida akielekea Washington.

Baadaye kwenye ujumbe, kupitia mtandao wa kijamii, Rais huyo wa Amerika alielezea matumaini kuwa hata mataifa ya China, Ufaransa, Korea Kusini, Uingereza miongoni mwa mengine, yatashiriki katika mpango huo.

Lakini jana Waziri Mkuu wa Japan Sanae Takaichi alisema nchi yake, ikiwa imebanwa na katiba yake inayopinga vita, haina mipango ya kutuma meli za kivita kusindikiza meli za kusafirisha mafuta kupitia Mkondo wa Hormuz Mashariki ya Kati.

“Hatujafanya uamuzi wowote kuhusu kutuma meli za kivita Mashariki ya Kati. Tunaendelea kukadiria kile Japan inaweza kufanya kivyake na kile kinaweza kufanyika kulingana na sheria iliyoko,” Takaichi akaambia bunge.

Kwa upande wake Australia, mshirika mwingine wa Amerika, ilisema kuwa haijapokea ombi lolote na haitatuma meli za kivita kusaidia katika kufunguliwa kwa mkondo huo hata ikipokea ombi hilo.

“Tunaelewa jinsi hatua hiyo ni muhimu zaidi. Lakini hatujaulizwa na hata kama tutapokea ombi hilo hatutakuwa tayari kutoa mchango wetu,” Catherine King, mwanachama wa baraza la mawaziri la Waziri Mkuu Anthony Albanese, akasema kwenye mahojiano na shirika la habari la kitaifa, ABC.

Rais Trump aliliambia gazeti la Financial Times Jumapili kwamba alitarajia China kusaidia katika kufunguliwa kwa Mkondo wa Hormuz kabla ya mkutano wake na Rais wa nchi hiyo Xi Jinping, jijini Beijing, mwishoni mwa mwezi huu.

Alidokeza kuwa huenda akaahirisha safari ya kwenda Beijing ikiwa China haitatoa usaidizi.

“Nadhani China pia inafaa kusaidia kwa sababu hupata asilimia 90 ya mafuta yake kupitia mkondo huo, Tunaweza kuchelewesha mkutano wetu na Xi ikiwa hawatatoa usaidizi hitajika,” Trump akaeleza.

Wizara ya Masuala ya Kigeni ya China haikujibu ombi la Reuters kuitaka kuzungumzia suala hilo.

Wakati huo huo, msemaji mmoja wa Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer alisema kiongozi huyo na Waziri Mkuu wa Canada walijadiliana na Trump kuhusu haja ya kufunguliwa kwa mkondo huo.

Lakini Korea Kusini ilisema itachunguza kwa makini ombi la Trump kuhusu suala hilo.

Tangu Amerika na Israeli ziliposhambulia Iran, Februari 28, Jamhuri hiyo ya Kiislamu imezuia meli kubwa za kusafirisha mafuta kupitia Mkondo wa Hormuz.