Wanafunzi waliochagua STEM Gredi 10 wakosa walimu waliohitimu kuwafundisha
WANAFUNZI wa Gredi 10 waliochagua masomo ya kiufundi katika shule za sekondari ya juu chini ya mkondo wa sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM) wamekaa bila kufundishwa tangu Januari kutokana na ukosefu wa walimu waliosomea taaluma hizo.
Huku zikisalia wiki mbili tu kabla ya Muhula wa Kwanza kuisha, walimu wakuu katika shule za sekondari ya juu wameelezea wasiwasi kuhusu upungufu wa walimu wataalamu katika masomo ya kiufundi chini ya mtaala mpya (CBE).
Masomo yaliyoathirika zaidi yanajumuisha sanaa ya vyuma, sayansi ya spoti, usafiri angani, ujenzi, stima, kilimo, masuala ya majini na uvuvi.
Masomo mengine yanayokosa walimu ni pamoja na Sanaa ya Ubunifu, Sayansi Kimu, Mandarin, Masomo ya Masuala ya Majini.
Kulingana na data kutoka Wizara ya Elimu, karibu asilimia 60 ya wanafunzi 1.2 milioni (takribani 677,144) wamesajiliwa kusomea mkondo wa STEM.
Hata hivyo, data inayoashiria mseto halisi wa masomo waliyochagua bado haijatolewa.
TSC inakadiria haja ya walimu 35,111 katika madarasa 15,046.
Sayansi Jamii inahitaji walimu 14,630 huku Sanaa na Spoti ikihitaji 8,778.
Upungufu wa walimu umelazimu shule kuajiri waelekezi wa kiufundi kupitia hazina zao mbalimbali za bodi za usimamizi (BoM), hivyo kusakama zaidi bajeti zao ndogo.
Muungano wa Walimu Wakuu wa Shule za Sekondari (KESSHA), ulisema changamoto kuhusu upungufu wa walimu inaathiri shule zote za sekondari ya juu.
“Tuna upungufu mkubwa wa wafanyakazi. Chini ya CBE, tunahitaji wataalam waliofuzu kwa masomo maalum kama vile usafiri angani, teknolojia ya majini, na ujenzi. Kwa sasa, hatuna wafanyakazi hawa. Sidhani kuna shule nchini iliyo na idadi kamili ya walimu hawa,” alisema mwenyekiti wa KESSHA, Willy Kuria.
Mkuu huyo wa KESSHA ambaye vilevile ni mwalimu mkuu wa Shule ya Upili ya Murang’a High, alifichua kuwa shule zinagharamika zaidi kuziba pengo hilo.