Habari za Kitaifa

Mkakati wa Ruto kupanga viongozi wa Kenya Kwanza wafichuliwa

Na JUSTUS OCHIENG March 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto anatekeleza mkakati unaochanganya mbinu za kisiasa na kiutawala ili kuleta vyama tanzu katika muungano wa Kenya Kwanza chini ya chake cha UDA.

Hatua hiyo inalenga kujiimarisha kisiasa na kuongeza nafasi ya kuchaguliwa tena katika Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Kwa mujibu wa vyanzo vya ndani ya serikali na muungano huo, mkakati huo mpana unalenga kuunda chombo imara cha kisiasa kitakachoweza kukabiliana na shinikizo kutoka kwa upinzani, hasa muungano wa upinzani unaoongozwa na Rigathi Gachagua na makundi mengine.

Taarifa zinaonyesha kuwa Rais Ruto amefanya mikutano kadhaa na viongozi wa vyama mbalimbali vilivyo ndani ya Kenya Kwanza.

Katika mikutano hiyo, anaripotiwa kuwaahidi nafasi muhimu ndani ya UDA, uteuzi serikalini na msaada wa kisiasa wakati wa uchaguzi ili kuhakikisha wanashinda wapinzani wao.

Muungano wa Kenya Kwanza unajumuisha vyama kadhaa vya kisiasa vyenye ushawishi katika maeneo tofauti ya nchi.

Miongoni mwa vyama hivyo ni Democratic Party of Kenya (DP) na Farmers Party ambavyo baadaye vilijiunga na upinzani. Pia kuna Ford-Kenya pamoja na Communist Party of Kenya.

Vyama vingine katika muungano huo ni National Agenda Party of Kenya, UDM, Economic Freedom Party na Chama Cha Mashinani.

Muungano huo ulihusisha Amani National Congress (ANC) ambayo baadaye ilivunjwa, pamoja na Devolution Party, Maendeleo Chap Chap, Grand Dream Development Party na TSP.

Vyama vingine ni Chama Cha Kazi, Tujibebe Wakenya Party, Pamoja African Alliance (PAA) na Umoja na Maendeleo Party.

Juhudi za kuunganisha vyama hivi pamoja faraghani ndizo nguzo kuu za mkakati wa Rais Ruto wa kuviweka chini ya mwavuli wa UDA.

Taarifa pia zinaonyesha kuwa katika juhudi zake za kuimarisha UDA, Rais Ruto amekuwa akijaribu kuvutia baadhi ya wanasiasa wenye ushawishi ndani yaODM, chama kinachohusishwa na kiongozi wa zamani wa upinzani marehemu Raila Odinga.

Wakati huo huo, baadhi ya vyama vya Kenya Kwanza bado vimesajiliwa rasmi katika ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa, lakini viongozi wao wamekubaliana kuunga mkono wagombeaji wa UDA katika uchaguzi wa 2027.

Spika wa Seneti Amason Kingi ambaye pia ni mwanzilishi wa chama cha PAA, amethibitisha kuwa chama chake hakitakuwa na wagombeaji katika uchaguzi huo.

Badala yake, waliotarajia kugombea kupitia PAA sasa watagombea chini ya UDA.

“Tulikutana na Rais Nairobi na tukajadiliana kuhusu jinsi ya kukabiliana na uchaguzi ujao kama kundi moja. Baada ya mashauriano na viongozi wa mashinani, tulikubaliana kwamba PAA haitakuwa na wagombeaji mwaka wa 2027,” alisema Bw Kingi.

Wachambuzi wa siasa wanachukulia hatua hii kama sehemu ya mkakati wa Rais Ruto wa kurahisisha usimamizi wa wagombeaji chini ya chama kimoja, hatua inayolenga kupunguza migogoro ya ndani inayotokea mara nyingi katika miungano ya vyama vingi.

Kuvunjwa kwa ANC na kukiunganishwa na UDA ni mojawapo ya hatua kubwa zaidi katika mpango huo, iliyobadilisha sura ya siasa katika eneo la Magharibi mwa Kenya na pia hesabu ya kisiasa ya Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi.

Hata hivyo, baadhi ya wachambuzi wanasema kuwa mkakati huo unaweza kuwa na faida za muda mfupi kisiasa lakini pia unaweza kudhoofisha mfumo wa vyama vingi nchini.

Wengine, akiwemo Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, wameonya kuwa kuvunja vyama kunaweza kudhoofisha demokrasia ya vyama vingi.

Kwa sasa, mapambano ya kisiasa ndani ya vyama shirika yanaendelea.

Ndani ya Maendeleo Chap Chap, Waziri wa Leba Alfred Mutua anakabiliana na mvutano baada ya baadhi ya wanachama wake wakiongozwa na Mbunge wa Kibwezi Magharibi Mwengi Mutuse kuanza kuhamia UDA.