Ripoti yafichua madiwani wanatumia karibu bilioni kutalii dunia kaunti zikikosa pesa
KAUNTI 41 nchini zilitumia jumla ya Sh822 milioni kwa safari za nje ya nchi ndani ya kipindi cha miezi sita, licha ya hatua za kubana matumizi zilizotangazwa na Rais William Ruto miaka miwili iliyopita.
Ripoti mpya ya Mdhibiti wa Bajeti Margaret Nyakang’o inaonyesha kuwa mafunzo na ziara za kujifunza zilikuwa sababu kuu zilizotumiwa kuhalalisha safari hizo, huku mabunge ya kaunti yakiongoza kwa matumizi makubwa zaidi.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Kaunti ya Lamu ndiyo iliyotumia fedha nyingi zaidi, ikitumia Sh65.4 milioni kuwasafirisha maafisa wake kwenda Arusha mara tano kwa mafunzo kuhusu usimamizi na uwajibikaji.
Cha kushangaza ni kwamba kiasi hicho ni zaidi ya Sh23 milioni kuliko fedha zilizotumiwa na serikali ya kaunti hiyo kwa shughuli za maendeleo, ambazo zilitumia Sh41.6 milioni katika kipindi hicho hicho.
Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa ni kaunti sita pekee—Homa Bay, Kwale, Isiolo Siaya, Mandera na Murang’a ambazo hazikutumia fedha zozote kwa safari za nje katika kipindi cha miezi sita.
Kwa ujumla, mabunge ya kaunti yaliongoza kwa matumizi ya safari hizo, yakitumia zaidi ya Sh511 milioni, sawa na zaidi ya asilimia 62 ya jumla ya fedha zilizotumika kwa usafiri wa nje.
Katika kipindi hicho, serikali za kaunti kupitia idara tofauti zilitumia zaidi ya Sh310 milioni kusafirisha maafisa wao nje ya nchi.
Miongoni mwa maeneo yaliyotembelewa zaidi ni Milki ya Kiarab, Singapore na Arusha.
Mabunge ya kaunti za Meru, Nakuru, Bomet na Tana River yalikuwa miongoni mwa yaliyotumia fedha nyingi zaidi kwa safari za kimataifa.
Bunge la Kaunti ya Meru lilitumia Sh63.72 milioni kufanya safari 18 za nje ya nchi, zikiwemo Arusha mara nne, Dubai mara nane, pamoja na ziara katika Ujerumani, Uturuki, Singapore mara mbili, Uganda na Ethiopia.
Bunge la Kaunti ya Nakuru lilitumia Sh47.7 milioni kwa safari za mafunzo katika Tanzania mara nane na Singapore mara mbili kati ya Agosti na Oktoba 2025.
Kwa upande wake, Bunge la Kaunti ya Bomet lilitumia Sh31.66 milioni kwa safari katika Angola, Brazil, Australia, Zanzibar, Spain na France.
Bunge la Kaunti ya Tana River nalo lilitumia Sh30.57 milioni kwa safari za Dubai kwa kongamano la uongozi na utawala bora, pamoja na mikutano ya maendeleo barani Afrika nchini India mara mbili na Uganda mara moja.
Ufichuzi huo unapatikana katika ripoti ya utekelezaji wa bajeti ya serikali za kaunti kwa nusu ya kwanza ya mwaka wa kifedha unaomalizika Juni 30, 2026.
Matumizi hayo makubwa yanaendelea licha ya serikali za kaunti mara nyingi kulalamikia ukosefu wa fedha unaodaiwa kuathiri utoaji wa huduma kwa wananchi.
Wakati huo huo, Baraza la Magavana limekuwa likishinikiza kaunti zitengewe zaidi ya Sh530 bilioni kama mgawo wa mapato katika mwaka ujao wa kifedha.
Mabunge ya kaunti yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara mbele ya Kamati ya Fedha na Bajeti ya Seneti, yakitaka kuongeza viwango vya bajeti yao pamoja na kupatiwa uhuru mkubwa wa kifedha.
Ripoti hiyo inaonyesha pia safari nyingi katika kaunti nyingine, zikiwemo Nyeri, Laikipia, Kitui, Trans Nzoia, Kajiado na Garissa, ambapo maafisa walitembelea mataifa mbalimbali kwa mafunzo na makongamano.
Kwa mfano, Bunge la Kaunti ya Kiambu lilitumia Sh13.3 milioni kwa safari za Tanzania mara tatu na nyingine kwenda Boston, Amerika.