Ufugaji nyuki kwa kutumia mbinu za kisasa unavyomuingizia mamilioni
UZOEFU wa miaka 12 wa Joseph Karuga katika sekta ya kilimo na mifugo umemchochea kubadilisha tasnia ya ufugaji nyuki nchini Kenya, hatua ambayo sasa inamwingizia mamilioni ya pesa.
Awali, Karuga alifanya kazi katika sekta ya mazao na ufugaji nyuki kwenye kampuni mbalimbali.
Kadri muda ulivyosonga, aligundua kuwa ufugaji nyuki una mianya mingi ya ufanisi lakini bado haujaangaziwa ipasavyo.
“Takwimu zinaonyesha kuwa Kenya inazalisha asali inayotosheleza karibu asilimia 20 tu ya mahitaji ya walaji. Hii inaonyesha wazi kuwa kuna pengo kubwa ambalo halijaangaziwa,” anaeleza.
Anasema pengo hilo lilimvutia kuingia katika sekta hiyo kwa lengo la kuibadilisha kupitia teknolojia za kisasa, hasa kwa kuwapatia wakulima mizinga iliyoboreshwa.
Karuga ni mwanzilishi mwenza wa Agriwell Kenya Limited, kampuni iliyoanzishwa mwaka 2022 inayotengeneza mizinga ya kisasa inayojulikana kama Langstroth.
“Niligundua changamoto kubwa inayokwamisha mafanikio ya sekta ya ufugaji nyuki ni ukosefu wa teknolojia za kisasa. Wafugaji wengi bado wanatumia mizinga ya zamani,” anasema.
Licha ya ufugaji nyuki kuwa huduma zilizoanzishwa kitambo, bado unategemea mbinu za jadi katika uzalishaji na uvunaji wa asali, hali inayopunguza ubora na kiwango cha uzalishaji.

Kwa kutumia mizinga ya kienyeji, mkulima huvuna mara moja au mbili kwa mwaka, huku mchakato wa uvunaji ukiathiri ubora wa asali.
Hata hivyo, kupitia mizinga ya kisasa iliyoboreshwa, mkulima anaweza kuvuna hadi mara tano kwa mwaka.
Wazo la kutengeneza mizinga, Karuga anasema lilitokana na changamoto ya upatikanaji mdogo wa asali alipoingilia biashara ya uuzaji. “Hatukuwa tunapata asali ya kutosha kwa sababu wakulima wengi walikuwa wanatumia mizinga ya kienyeji,” anakumbuka.
Kwa mtaji wa Sh1.5 milioni—ikiwemo Sh850,000 kutoka akiba ya waanzilishi wa Agriwell Kenya Limited, na mkopo—walijitosa katika utengenezaji wa mizinga ya Langstroth.
Ndani ya miaka mitatu, biashara ya wajasiriamali hao imekua kwa kasi. Kutoka kutengeneza mizinga 30 kwa mwezi, sasa wanaunda kati ya 300 hadi 500, na wakati oda zinakuwa nyingi hadi mizinga 1,000.
Kampuni ya Karuga na mwanzilishi mwenza ina karakana kando ya Barabara ya Eastern Bypass, Ruiru, Kaunti ya Kiambu, pamoja na kituo cha kuchakata asali.
Kufikia mwisho wa 2024, walikuwa wamefanya kazi na zaidi ya wafugaji nyuki 3,200 kote nchini.
“Tunauza mizinga na pia kuunganisha wafugaji na soko la asali. Aidha, tunanunua kilo moja kwa Sh500 na kuuza kati ya Sh800 hadi Sh1,000,” akaamia Akilimali Dijitali wakati wa mahojiano.

Mzinga mmoja wa Langstroth unaweza kuzalisha kati ya kilo 10 hadi 15 za asali. Bei ya mzinga mmoja ni kati ya Sh5,500 na Sh9,000 kulingana na ubora.
Mbali na uundaji wa mizinga, Agriwell pia husambaza vifaa vya kujikinga wakati wa uvunaji, uvunaji asali, na mafunzo bora kwa wafugaji.
Kampuni yetu, Karuga anasema, inalenga hasa vijana na wanawake ili kuongeza uzalishaji, kwani sekta ya ufugaji nyuki bado inaongozwa na wanaume wazee.
Kwa mujibu wa Idara ya Maendeleo ya Mifugo, Kenya ina uwezo wa kuzalisha tani 100,000 za asali kwa mwaka, lakini huzalisha tani 17,000 pekee. Ni gapu kubwa inayoashiria sekta yenye mianya tele kimapato.
Licha ya changamoto kama ukosefu wa miundomsingi thabiti na ushuru wa juu, Karuga anaendelea kusonga mbele na kuimarika.
Pia, binafsi anafuga nyuki ambapo ana mizinga 200 katika maeneo ya Sagana, Naivasha na Nyandarua.
Anasema ufugaji nyuki umemfundisha nidhamu na uvumilivu, huku akiamini kuwa kupitia ubunifu na teknolojia sahihi, sekta hiyo inaweza kuwa chanzo kikubwa cha ajira kwa vijana na kipato.