Amebobea kuchoma nyama kwa kutumia moshi
KILICHOANZA kama burudani ya kupikia familia na marafiki nyumbani karibu miaka kumi iliyopita kwa Steve Gitu, sasa kimegeuka kuwa fursa kubwa ya kibiashara.
Leo hii, Gitu ni mwanzilishi wa Rib Racks Ltd, kampuni inayojihusisha na uchomaji wa nyama na bidhaa mbalimbali za nyama.
Gitu anadokeza kwamba alianza na kituo kimoja cha kuchoma nyama jijini Nairobi, lakini sasa amepanua biashara hiyo na anaendesha matawi matano.
Mjasiriamali huyu aliyelelewa katika familia iliyozamia biashara ya uuzaji nyama, ana uwepo Nakuru, Naivasha, Kiambu Road, Kamakis pembezoni mwa Eastern Bypass Ruiru, na Karen kando ya barabara ya Lang’ata, Nairobi.
Utaalamu wake mkuu ni uchomaji wa nyama kwa mtindo wa Barbecue (BBQ). BBQ, maana yake ni mfumo wa kupika nyama polepole kwa kutumia kiwango cha chini cha joto. Kwa kawaida hutumia moshi kutoka kwa kuni au makaa, na upikaji huu wa polepole hufanya nyama iwe laini na kuipa ladha tamu ya moshi.
“Nyama tunayopika kupitia mtindo wa BBQ ni ya ng’ombe, kondoo, mbuzi, nguruwe na kuku,” Gitu anasema.

Hali kadhalika, amebobea kuchoma vipande maalum vya nyama kama mbavu (ribs), Sanchez, pamoja na bidhaa zilizochakatwa kama vile soseji, bacon, burger, michuzi, na viungo vingine vya mifugo.
Kutoka kuchoma kilo chache za nyama kwa wiki, Gitu sasa anajivunia kuchoma zaidi ya tani moja ya nyama.
Tofauti na kuchoma nyama kwa haraka – kwa joto kali na la juu, Gitu anakiri kwamba mbinu ya BBQ husaidia kulainisha nyama na kuongeza ladha. Anaeleza kuwa mfumo huu wa aina yake umemwezesha kuwahi soko lenye ushindani mkuu, kinyume na ule wa “nyama choma ya kawaida.”
Mafanikio yake yalianza kwa kuburudisha familia na marafiki, kabla ya kuangazia fursa ya kibiashara kupitia huduma za upishi katika hafla za kibinafsi kama vile harusi.
“Familia yangu pia imekuwa kwenye biashara ya nyama kwa muda mrefu, hivyo basi si jambo geni kwangu,” akaambia Akilimali Dijitali kwenye mahojiano ya kipekee.
Anafichua kwamba nyanya yake ambaye alikuwa na bucha Kenyatta Market, Nairobi alimfundisha jinsi ya kuendesha biashara ya nyama.

“Baada ya kutafuta ajira kwa miaka mitano bila mafanikio, niliamua kurejea katika biashara ya familia,” anaeleza.
Gitu anasema ubunifu wake katika mapishi ndio unaovutia wateja wengi. “Wakenya wanapenda nyama. Ukiiongezea ladha, wanaongezeka mara dufu.”
Rib Racks Ltd ilizinduliwa rasmi mwaka 2018, kwa mtaji wa Sh800,000. Kutoka kuanza peke yake, sasa ameajiri zaidi ya watu 150. Biashara hiyo pia imeunda ajira zisizo za moja kwa moja kwa wafugaji kutoka Kajiado na Narok, pamoja na wasambazaji wa mifugo kutoka Kiambu.
Changamoto kubwa mwanzoni ilikuwa ukosefu wa wafanyakazi wenye ujuzi, lakini sasa amewekeza kwa wataalamu na mifumo bora ya usimamizi. Kuboresha biashara yake, ameshirikiana na Ahmad Suleiman wa Old Lake Meatery Ltd, anayemsambazia bidhaa kama vile soseji na pia kusaidia kusaka masoko.
Somo lake kuu kwenye biashara? “Lazima uwe tayari kufanya chochote—na pia kuwa tayari kupoteza chochote.”