Afya na Jamii

Asilimia 87 ya Wakenya wanatatizika kifedha na kiakili, utafiti waonyesha

Na HELLEN SHIKANDA March 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KWA muda wa miezi tisa, Emily (si jina lake halisi) aliendelea kwenda kazini akitumaini mwajiri wake angemlipa mshahara wake mwisho wa mwezi.

Lakini siku ya malipo ilipowadia, hakupokea taarifa yoyote kutoka benki.

Mwajiri wake aliendelea kutoa ahadi kwamba mwezi ujao hali ingeboreka na malimbikizi yote ya mishahara yangelipwa kikamilifu.

Emily anafanya kazi katika shirika la barabara linalohusishwa na serikali, na kwa kuhofia kunyanyaswa kazini, aliomba jina lake lisitajwe.

Emily alisoma kwa bidii na kufuzu kusomea uhandisi.

Sasa ni mhandisi wa kiwango cha kati aliyeidhinishwa, lakini amejikuta akihangaika kujikimu kutokana na changamoto za kifedha na fursa chache za ajira katika taaluma yake.

“Mapato yako yakiwa si ya uhakika, akili yako hubaki katika hali ya kupambana ili kuishi. Ninapata msongo wa mawazo kwa sababu ninahofia jinsi nitakavyolipa bili bila kipato,” anasema.

Katika shirika hilo hilo lakini tawi tofauti, Bernard (si jina halisi), amekumbwa na hali hiyo kwa miezi sita iliyopita.

Siku moja kabla ya kuzungumza na Taifa Leo, alipokea simu kutoka benki iliyompa mkopo, ikimtaka aanze kulipa.

“Nilipaswa kulipa mkopo huo kwa miezi mitatu, kuanzia Desemba hadi Februari. Sikufanya hivyo. Nilimweleza tu mhudumu aliyenipigia, naye akaelewa,” anasema.

Bernard hajui hali hiyo itaendelea kwa muda gani, wala benki itaendelea kuwa na uvumilivu kwa muda gani.

Anaendelea kwenda kazini kila siku, lakini anasema motisha imepungua sana.

Bernard na Emily wanawakilisha Wakenya wengi, takriban asilimia 87, wanaokumbwa na msongo wa kifedha unaoathiri afya yao ya akili, kulingana na ripoti mpya iliyotolewa wiki hii na shirika la Cigna Healthcare Middle East and Africa.

Ripoti hiyo inaonyesha kuwa Wakenya wengi sasa wako tayari kuzungumzia matatizo yao ya afya ya akili, lakini viwango vya msongo vimeongezeka ikilinganishwa na mwaka 2024, ambapo asilimia 84 waliripoti kuwa na msongo.

Gharama ya juu ya maisha na ukosefu wa fedha vinatajwa kuwa sababu kuu.

Licha ya msongo huo, Wakenya pia wanaonyesha ustahimilivu, wakitegemea familia, afya ya mwili na imani ya kiroho.

Utafiti huo ulihusisha takriban watu 13,000 kutoka Kenya na mataifa mengine duniani.

Ripoti hiyo inaonyesha kuwa ustawi wa kifedha ni dhaifu zaidi kwa Wakenya, huku vijana wa miaka 18 hadi 24 wakiripoti viwango vya juu zaidi vya msongo wa mawazo.

Athari zake ni pamoja na kukosa usingizi, kujitenga kijamii na kuwa na hisia kali kupita kiasi.

Mwanasaikolojia Silas Kiriinya, anasema watu wanapoenda kazini wanatarajia kupata malipo mwisho wa mwezi, na hali hiyo isipotekelezwa, motisha huporomoka na kazi yenyewe huwa chanzo cha mafadhaiko.

“Katika kipindi hiki, mahusiano yanaweza kuvunjika kutokana na matatizo ya kifedha, jambo linaloongeza changamoto za kiakili,” anasema.

Anaongeza kuwa msongo wamawazo wa muda mrefu unaweza kusababisha magonjwa ya mwili kama vidonda vya tumbo, maumivu ya kichwa na matatizo ya kusaga chakula.

Wengine hujikuta wakikimbilia tabia kama ulevi, hali inayozidisha matatizo yao.

Anasisitiza kuwa mashirika yanapaswa kujali ustawi wa wafanyakazi wao kwa ujumla.

“Kumfanyia mfanyakazi hivi ni kumwangamiza, si kifedha tu, bali pia kiakili, na hilo huathiri uzalishaji kwa muda mrefu,” anasema.

Anashauri wafanyakazi katika hali hiyo kutafuta usaidizi wa kitaalamu au wa kiroho, na pia kujifunza ujuzi mpya ili kupata vyanzo mbadala vya mapato.

Utafiti unaunga mkono uhusiano kati ya msongo wa kifedha na afya.

Tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa afya ya akili ni muhimu katika utendaji kazini na inaweza kusababisha watu kuacha ajira mapema ikiwa hautashughulikiwa.

Utafiti mwingine uliochapishwa katika jarida la BMC Public Health uligundua kuwa hata wasiwasi mdogo wa kifedha unaweza kuongeza uwezekano wa msongo wa kisaikolojia, huku msongo wa muda mrefu ukichangia dalili za mafadhaiko.

Utafiti huo unaonyesha kuwa msaada wa kijamii kutoka kwa familia na marafiki husaidia kupunguza msongo wa mawazo.

“Tunapohisi kuungwa mkono na kuwa na uwezo wa kuukabili, msongo hupungua,” utafiti huo unasema.