Utafutaji mahari ndio unachangia wizi wa mifugo, Waziri Murkomen asema
WIMBI la ujangili na wizi wa mifugo lililosababisha vifo vya watu wengi na kuibwa kwa maelfu ya mifugo linachochewa na shinikizo za kitamaduni kwa vijana wanaotaka kuoa.
Waziri wa Usalama wa Ndani, Bw Kipchumba Murkomen, alisema visa vya wizi wa mifugo ambavyo vimekuwa vikikumba kaunti za Meru, Laikipia, Isiolo, Marsabit na Samburu kwa miaka mingi, vinatekelezwa na vijana wanaohitaji ng’ombe kwa ajili ya mahari.
Waziri huyo alizungumza Jumatatu akiwa Mbataru eneo la Tigania Mashariki, ambapo aliwahakikishia viongozi kuwa serikali imejitolea kukomesha uhalifu huo.
Ziara hiyo imejiri baada ya ongezeko la visa vya wizi wa mifugo ambavyo vimesababisha vifo vya watu 11 na kuibwa kwa zaidi ya ng’ombe 600 katika miezi miwili iliyopita.
Bw Murkomen alisema maafisa 400 wa polisi wametumwa katika eneo la Meru Kaskazini mpakani mwa Kaunti ya Isiolo ili kukabiliana na uhalifu huo.
Aliongeza kuwa maafisa hao watasaidia kurejesha utulivu kabla ya operesheni ya kukusanya silaha haramu.
Aidha, alisema kuwa askari wa akiba wa polisi 125 wataajiriwa na kutumwa eneo hilo ili kuimarisha usalama.
“Tutawafuata majangili, wafadhili wao pamoja na wale wanaowawezesha ndani ya mfumo wa usalama. Mpango wetu ni kutuliza eneo hili na kurejesha amani,” alisema Bw Murkomen.
Alisema kikosi cha pamoja cha usalama kitaendelea na operesheni hadi mifugo yote iliyoibwa na silaha haramu zitakapopatikana.
“Isiolo, tumetwaa bunduki haramu 30 tangu Februari mwaka huu. Katika maeneo ya Baringo na Elgeyo Marakwet, zaidi ya bunduki 1,200 zimetwaliwa tangu operesheni ianze. Lengo letu ni kuhakikisha silaha zote zinarejeshwa,” aliongeza.