Familia za vijana waliofia vitani Urusi zazika migomba baada ya kuelezwa miili haitaletwa
KABLA ya kujibwaga katika uwanja wa vita Ukraine, James na Charles hawakuwa wamefahamiana.
Walikuwa vijana wawili kutoka familia tofauti, wakisukumwa na ndoto za maisha bora nje ya nchi.
Lakini bila wao kujua, safari yao ya matumaini iliishia kuwa tiketi ya mauti katika vita ambavyo hawakuwa na uhusiano navyo.
Na sasa, familia zao zinazika migomba baada kupoteza matumaini ya kupata mili yao.
Wote wawili waliingia Urusi wakiamini wangefanya kazi za kawaida kama upishi au udereva.
Ahadi ya mishahara minono na maisha bora iliwaongoza kufanya uamuzi huo. Hata hivyo, muda mfupi baadaye, walijikuta wakiwa sehemu ya jeshi, wakikabiliana na hatari za vita.
Leo hii, wote wamefariki na hata katika kifo, familia zao hazijawahi kuonana wala kushirikiana katika maombolezo.
Jambo la kusikitisha zaidi ni kwamba, miili yao haijarejeshwa nyumbani.
Familia zimebaki na chaguo mbili ngumu kutoka kwa mamlaka za Urusi— miili ichomwe na majivu kurejeshwa, au izikwe huko kwa heshima za kijeshi.
Kwa familia nyingi za Kiafrika, uchomaji maiti ni kinyume na mila, na kuzikwa mbali na nyumbani ni pigo lingine kihisia.
Kutokana na hali hiyo, familia zimelazimika kufanya mazishi mwigo, zikizika migomba badala ya miili ya wapendwa wao.
Ni njia ya kutafuta faraja, ingawa haizibi pengo la maumivu.
Kwa familia ya James, huzuni bado ni nzito. Dada yake Margaret anasema mama yao bado hajakubali kuwa mwanawe hayuko tena.
James alikuwa mtoto wa kipekee katika familia yao ndogo, akiwa na ndoto ya kununua ardhi na kusaidia mama yake.
Dakika chache kabla ya kuondoka Kenya, alimwambia dada yake kuwa angeenda kubadilisha maisha yake.
Hakuwa mtu wa kuzungumza sana, lakini ndoto zake zilikuwa kubwa.
Kwa upande wa Charles, mama yake Bibiana Waithaka anaishi katika majonzi yasiyoelezeka.
Aliamini mwanawe angepata kazi yenye mshahara wa hadi Sh800,000 kwa mwezi. Badala yake, hali ilibadilika ghafla na akajikuta akiomba pesa kutoka nyumbani ili kuishi.
Simu yake ya mwisho ilikuwa ya kutisha—alianza kusema “Mama, mama leo…” akilia kabla ya simu kukatika.
Hiyo ndiyo ilikuwa sauti yake ya mwisho.