Gachagua: Nina taarifa SHA haina pesa, na itaporomoka ndani ya miezi sita
ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua ameonya kuwa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA) iko katika hatari ya kuporomoka, akidai kuwa mpango huo wa bima ya afya unaoendeshwa na serikali unaweza kukumbwa na changamoto kubwa katika miezi sita ijayo.
Akizungumza katika Kanisa la ACK Dayosisi ya Kirinyaga, eneo la Ndia, Jumapili, Bw Gachagua alieleza wasiwasi kuhusu mfumo huo wa afya nchini, akionya kuwa iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa, kuporomoka kwa SHA kunaweza kusababisha changamoto kubwa katika utoaji huduma za afya nchini.
“Nina taarifa kuwa SHA itaporomoka ndani ya miezi sita na tutakuwa na shida katika sekta ya afya,” alisema.
Kulingana na Gachagua, madeni ambayo SHA inadaiwa na hospitali, hasa zile za kidini na za kibinafsi, yanaathiri pakubwa mfumo mzima wa afya.
Alisema kwa sasa, hospitali hizo zinadai mabilioni ya fedha na hali hiyo inaweza kuzifanya zifunge shughuli zao.
“Leo tunavyozungumza, hospitali zetu, hasa zile za kidini, zinadai SHA takriban Sh90 bilioni na ziko karibu kufungwa,” aliongeza.
Alionya kuwa iwapo SHA itaporomoka, athari zake zitakuwa kubwa na kuathiri hospitali zote nchini.
“Nataka kuonya kuwa ikiwa SHA itaporomoka, hospitali zote zitaporomoka. Hospitali zinapaswa kudai malipo kabla ya kutoa huduma,” alisema.
Kauli zake zinajiri wakati ambapo SHA inakabiliwa na changamoto za kifedha, huku hospitali zikidai madeni yanayokadiriwa kufikia Sh76 bilioni, ikiwa ni pamoja na madeni yaliyorithiwa kutoka kwa Hazina ya Bima ya Afya ya Taifa (NHIF) iliyofutwa.
Hata hivyo, serikali imeanza kulipa sehemu ya madeni hayo. Mnamo Machi, serikali ilitoa Sh15.4 bilioni kwa hospitali, pamoja na Sh4.1 bilioni zaidi kusaidia kulipa sehemu ya madeni ya NHIF.
Shinikizo
Licha ya malipo hayo, hospitali zimeendelea kushinikiza serikali kulipa fedha zaidi, hali ambayo Gachagua anaonya inaweza kusababisha kufungwa kwa baadhi ya vituo vya afya endapo hali itaendelea kuwa mbaya.
Ili kukabiliana na hali hiyo, kiongozi huyo wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP) alipendekeza kuwa hospitali zibadili mfumo wa malipo kwa kudai fedha mapema badala ya kusubiri malipo yanayocheleweshwa.
“Napendekeza hospitali zianze kudai malipo kutoka kwa SHA kabla ya huduma. Zikadirie matumizi ya kila mwezi na zilipwe mapema,” alisema.
Kwa mujibu wake, hatua hiyo itasaidia kulinda uthabiti wa kifedha wa hospitali na kuhakikisha huduma za afya zinaendelea bila kukatizwa.
Hata hivyo, Waziri wa Afya Aden Duale amepuuza madai ya Gachagua, akisema yanachochewa na siasa badala ya ukweli wa hali ilivyo.
Akizungumza katika hafla ya kuchangisha fedha jijini Nairobi, Duale alimshutumu Gachagua kwa kueneza hofu miongoni mwa wananchi na kujaribu kunufaika kisiasa kutokana na mjadala wa SHA.