Habari za Kitaifa

Gavana ajitenga na kisa cha miili 33 kutoka Nyamira kuzikwa Kericho, akemea ‘maafisa wafisadi’

Na RUTH MBULA, VITALIS KIMUTAI March 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KUZIKWA kisiri kwa miili 33 katika Kaunti ya Kericho kumechukua sura mpya huku Gavana wa Nyamira, Amos Nyaribo, akilaumu baadhi ya maafisa wa serikali yake kwa ufisadi na watu wanne zaidi wakikamatwa kuhusiana na kisa hicho.

Akizungumza jana, gavana huyo alijitenga na mazishi hayo na kusema maafisa waliohusika “watabeba msalaba wao wenyewe.”

Alifichua kuwa afisa aliyepewa jukumu la kusafirisha miili alikosa kutuma fedha zilizotolewa kwa shughuli hiyo kwa Serikali ya Kaunti ya Kericho, na badala yake akazika miili hiyo katika makaburi ya kibinafsi.

“Miili ilikuwa imepangwa kuzikwa kwenye kaburi la umma na afisa aliyepewa kazi hiyo alipewa Sh 32,000 ambazo zingelipwa serikali ya kaunti. Badala yake, afisa huyo alitumia mhudumu wa mochari sehemu ya fedha hizo,” alisema Gavana Nyaribo.

Aliongeza: “Miili ilikuwa imepangwa kuzikwa mchana. Hatuna siri yoyote. Tuachie polisi wafanye uchunguzi na kufichua ukweli.  Tulituma gari na afisa kupeleka miili 13, lakini kilichofuata bado kinachunguzwa.”

Waziri wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen, jana alieleza wasiwasi wake kuhusu kufichuliwa kwa kaburi la pamoja Kericho, ambapo watu sita walikamatwa.

“Kuna amri ya mahakama iliyoelekeza idadi ya miili isiyopasa kuzikwa. Haikufaa kufanyika gizani,” alisema Waziri, huku akiongeza kuwa maafisa wa Nyamira walihusika katika kupanga mazishi hayo kwa siri, labda kwa faida ya kifedha.

Kwa mujibu wa ripoti, miili hiyo inajumuisha watoto 25 na watu wazima 8, pamoja na sehemu za miili, jambo linaloongeza maswali kuhusu hali ya mazishi hayo.

DCI inachunguza chanzo cha miili mingine 20, huku awamu ya kwanza ya uchunguzi ikithibitisha kuwa baadhi ya miili ilitoka Nyamira.

Sheria ya Kenya inasema kuwa hospitali zinaweza kuzikwa miili isiyodaiwa baada ya siku 14 kwa kutumia amri ya mahakama.

Gavana Nyaribo alikaribisha uchunguzi huo, akisisitiza dhamira ya utawala wake ya kubaini asili ya miili mingine 20 na hali ya mazishi.

“Tunataka kujua ni wapi miili mingine ilitoka,” alisema, akiwahimiza wananchi kuwaacha wachunguzi wafanye kazi yao bila ushawishi. Washukiwa wamezuiliwa katika vituo mbalimbali vya polisi Kaunti ya Kericho. Waziri Murkomen alilaani mazishi hayo ya siri, akisema ni kinyume cha sheria.

“Wote waliohusika watachukuliwa hatua za kisheria kikamilifu,” alisema.