Gavana Nassir ataka viongozi wa Linda Mwananchi waondoke ODM
GAVANA wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir, amewataka wanasiasa wanaoegemea mrengo wa Linda Mwananchi waondoke katika Chama cha ODM iwapo hawataki kufuata msimamo wa chama hicho.
Akizungumza Jumapili alipozuru maeneo ya Jomvu, Bw Nassir alisema wanasiasa hao tayari wameonyesha nia ya kuunda chama chao na hivyo basi itakuwa vyema wakijitenga na ODM mapema hii.
“Kama hutaki kufuata msimamo wa chama cha ODM, basi ondoka. Tunajua wazi ya kuwa mmeunda chama chenu na karibuni itadhihirika wazi,” alisema.
Wakati Bw Nassir akifanya mkutano wake, mrengo huo wa Linda Mwananchi ukiongozwa na Seneta wa Nairobi, Bw Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya, Bw James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki, Bw Babu Owino, miongoni mwa wengine ulifanya mkutano wa hadhara katika uwanja wa Tononoka, uliohudhuriwa na umati mkubwa.
Katika mkutano huo, baadhi ya viongozi waliohutubu waliashiria kwamba watatoa ‘tangazo kubwa’ kuhusu mwelekeo watakaochukua kisiasa hivi karibuni.
Bw Nassir, ambaye pia ni Naibu Kinara wa ODM alitoa wito kwa wanachama kuunga mkono mchakato wa mazungumzo rasmi kati ya chama hicho na UDA Uchaguzi Mkuu wa 2027 unaponukia.
Alisema ODM imempa fursa rasmi kinara wa chama hicho, Dkt Oburu Oginga, aanze mazungumzo chama tawala cha UDA kinachoongozwa na Rais William Ruto.
“Tutakaa chini na UDA, na sisi tunasema ile idadi ya mawaziri tumepewa haitoshi. Tunataka Naibu Rais atoke kwenye chama chetu cha ODM,” aliongeza.