Hatua ya Uhuru na Gachagua kuchangamkiana hadharani yaibua gumzo la kushirikiana
HATUA ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta na Kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua kuchangamkiana hadharani kwenye mazishi Kaunti ya Kirinyaga jana imeibua mdahalo kuwa wawili hao wataridhiana na kuwa mrengo mmoja kwenye uchaguzi wa 2027.
Bw Kenyatta na aliyekuwa naibu rais jana waliketi sako kwa bako wakati wa ibada ya mazishi ya Seneta wa zamani wa Kirinyaga Daniel Karaba.
Hii ilikuwa mara ya kwanza ambapo viongozi hao wawili waliokuwa mahasimu wakali kuelekea uchaguzi wa 2022, walipokuwa wakijumuika kwenye hafla ya pamoja.
Uhuru na Gachagua walionekana wakizungumza, kufurahi na kuchangamkiana wakati wa ibada hiyo iliyohudhuriwa na vinara wengine wa upinzani.
Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, Martha Karua (PLP), Dkt Fred Matiangí (Jubilee), Eugene Wamalwa (DAP-Kenya) walihudhuria mazishi hayo.
Bw Kenyatta katika hotuba yake alimrejelea Bw Gachagua kama ‘Ndugu yangu..Riggy G kutoka Wamunyoro, kauli ambayo ilishangiliwa na waombolezaji.
“Nasikia watu wakisema wanasikiza watu wa chini na hata mimi nikiwa Ichaweri naisikiza lakini nataka nikwambie kuwa usimamie kile unachoamini. Mnamo 2022 ulifanya kosa na sasa unaumia. Sasa usiyarudie makosa hayo,” akasema Bw Kenyatta kwenye matamshi yaliyoonekana yalilenga wapigakura kutoka ukanda wa Mlima Kenya na pia kiongozi huyo wa DCP.
Bw Gachagua ambaye anaonekana kama kigogo wa siasa za Mlima Kenya alionekana kuridhia matamshi ya Bw Kenyatta huku akisisitiza ataendeleza maasi dhidi ya utawala wa sasa wa Rais William Ruto.
“Nani alisema ndugu hawawezi kuungana tena? Rais Ruto hajui jamii hii, tulimpa kura zetu na akafikiria yeye ni mmoja wetu na anatujua vizuri. Bw Kenyatta ni ndugu yangu mkubwa ambaye nina historia naye ambaye Ruto analenga kupaka tope,” akasema.
Uhasama kati ya Bw Gachua na rais mstaafu ulizingirwa na kamatakamata, kesi kortini, kujibizana hadharani na tofauti kali za kisiasa kuhusu ubabe wa siasa za Mlima Kenya.
Bw Musyoka ambaye analenga kura za Mlima Kenya alisema kuwa 2027 lazima Mabw Kenyatta na Gachagua wafanye kazi pamoja.
“Kuna watu ambao wanaamini hii haiwezekani. Sasa wameshanga na wanaweza kukutumia hata maafisa wa Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru (KRA) kukuhangaisha. Simama kidete,” akasema.
Bw Wamalwa naye alisema kuwa ilikuwa raha kuwaona Mabw Gachagua na Kenyatta wakiwa kwenye jukwaa moja na vinara wa upinzani na viongozi wa Linda Mwananchi.
Gavana wa Siaya James Orengo alisema kuwa maeneo mengine yanaungana na Mlima Kenya kuhakikisha Rais Ruto hachaguliwi tena 2027.
“Tuko na Mlima pamoja na Ruto lazima aende,” akasema Bw Orengo.