Shule zalaumiwa kuhusu usambazaji wa vitabu Gredi 10
USAMBAZAJI wa vitabu vya Gredi 10 nchini umekwama baada ya shule nyingi kukosa kuwasilisha taarifa muhimu kuhusu idadi ya wanafunzi na vitabu walivyopokea, hali inayozua wasiwasi kuhusu uwajibikaji.
Taasisi ya Ukuzaji wa Mitaala Kenya (KICD) imesema ni shule 1,213 pekee kati ya zaidi ya 23,000 ambazo zimewasilisha ripoti hizo, jambo linalochelewesha hatua ya pili ya usambazaji wa vitabu.
Mkurugenzi Mkuu wa KICD, Charles Ong’ondo, alisema changamoto kubwa ni data isiyo sahihi kutoka shuleni, ambayo imechangia baadhi ya shule kulalamikia upungufu wa vitabu huku nyingine zikiwa na ziada.
“Wakati mwingi tunapokea takwimu zisizo sahihi. Unapeleka vitabu shuleni na wanadai wanafunzi wao ni wengi kuliko ilivyoonyeshwa, lakini ni nadra shule kusema wana wanafunzi wachache,” alisema Profesa Ong’ondo.
Alifafanua kuwa orodha iliyotumika kusambaza vitabu iliandaliwa Septemba mwaka jana, hivyo idadi ya wanafunzi inaweza kuwa imebadilika kufikia wakati wa usambazaji.
Hali hii imechangia baadhi ya shule kutopokea vitabu au kupokea vichache.
KICD ilitangaza kuwa imekamilisha awamu ya kwanza ya usambazaji wa vitabu kwa shule za upili za umma na sasa inahitaji uthibitisho wa takwimu za wanafunzi ili kuongoza awamu ya pili.
Lengo ni kuhakikisha kila mwanafunzi anapata kitabu chake, kulingana na sera ya serikali.
Kwa mujibu wa takwimu, vitabu 11,867,325 viliagizwa na kuchapishwa, huku nakala 11,485,000 zikiwa tayari zimesambazwa, sawa na asilimia 96.78 kufikia Machi 27, 2026.
Kanda ya Kati na Nairobi zimefikia asilimia 100 ya usambazaji, huku Magharibi ikiwa na asilimia 98.01, Nyanza 96.94, Bonde la Ufa 96.66, Pwani 95.51, Mashariki 95.20 na Kaskazini Mashariki 91.92.
Hata hivyo, KICD imezitaka shule ambazo hazina wanafunzi au zilizo na ziada ya vitabu kutangaza idadi kamili na kuvirudisha v visambazwe upya. Taasisi hiyo imeweka kiunzi cha mtandao na nambari ya simu kwa shule kuwasilisha taarifa hizo.
“Tatizo hili linaweza kurekebishwa sasa, lakini tunahitaji ushirikiano wa shule kutoa taarifa sahihi na kurejesha vitabu vya ziada ili vipelekwe kwa shule zinazovihitaji,” alisema Profesa Ong’ondo.
Alionya kuwa kuchelewa kushughulikia tatizo hilo kunaweza kusababisha changamoto kubwa zaidi mwaka ujao wanafunzi watakapoingia Gredi 11.