Acha ngoma itambae! Makanisa kuendelea na kelele Mombasa wamiliki hoteli wakilalamika
HOTELI zilizo karibu na maeneo ya ibada jijini Mombasa zimepata pigo baada ya Mahakama ya Mazingira na Ardhi kubatilisha uamuzi uliokuwa umewalinda dhidi ya kelele na kutoka makanisa jirani.
Awali, Baraza la Mazingira (NET) katika uamuzi wake wa Novemba 19, 2024, lilipigia debe Darajani Hotel Ltd na Bridge Hotel Ltd kwa kutoa amri ya kudhibiti kelele kutoka kwa makanisa katika eneo hilo.
Baraza hilo liliagiza makanisa yaliyo karibu kudhibiti sauti za ibada ili zisivuke mipaka ya majengo yao na kuwasumbua wageni.
Uamuzi huo pia ungeweza kusherehekewa na hoteli nyingine zinazokumbwa na kelele kutoka makanisa.
Hata hivyo, mnamo Machi 19, Mahakama ya Mazingira na Ardhi jijini Mombasa ilibatilisha uamuzi huo na kuwaacha viongozi wa makanisa hayo waendelee na kelele zao.
Mahakama ilisema NET halikuwa na mamlaka ya kisheria kusikiliza kesi hiyo , na hivyo uamuzi wake wote kuwa si halali bila kujali kama ulikuwa sahihi au la.
Mahakama pia ilibaini kuwa udhibiti wa kelele hauko tena chini ya Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi wa Mazingira (NEMA), na hivyo rufaa zote zinazohusu masuala hayo haziwezi kushughulikiwa na NET.
Mgogoro huo ulianza hoteli hizo mbili zilipowasilisha malalamishi, zikilalamikia kelele nyingi kutoka makanisa jirani, yakiwemo Life Transforming Centre, ambazo zilikuwa zinaathiri biashara yao.
Hoteli hizo ziliishutumu NEMA kwa kutoshughulikia malalamishi yao chini ya Sheria ya Usimamizi na Uratibu wa Mazingira, na kudai kuwa kelele hizo zilisababisha kupungua kwa wateja na hasara ya kifedha.
NET ilikubaliana na hoteli na kuamuru makanisa kudhibiti sauti zao ili zisivuke mipaka ya majengo yao.
Pia iliamuru NEMA kufanya ukaguzi na kuwasilisha ripoti ya utekelezaji ndani ya siku 90.
Hata hivyo, mahakama hiyo haikutoa fidia kwa hoteli, ikisema ushahidi wa hasara haukuwa wa kutosha.
Makanisa yalipinga uamuzi wa NET, na kukata rufaa katika Mahakama ya Mazingira na Ardhi.
Yalisema kuwa NET haikuwa na mamlaka, na udhibiti wa kelele sasa ni jukumu lililogatuliwa chini ya Katiba ya Kenya.
Pia, yalidai kuwa vipimo vya kelele vilivyotumika havikuwa vya kuaminika na hawakupewa nafasi ya kutosha kusikilizwa kuhusu gharama za kesi.
Mahakama ya Mazingira na Ardhi ilibaini kuwa rufaa kwa NET lazima itoke kwenye masuala yaliyo ndani ya mamlaka ya NEMA, kama inavyoruhusiwa na Kifungu cha 129 cha Sheria ya Usimamizi na Uratibu wa Mazingira.
Mahakama ilisema kuwa kwa kuwa udhibiti wa kelele hauko tena chini ya NEMA, NET haikuwa na msingi wa kisheria kusikiliza kesi hiyo.
Mahakama pia ilibainisha kuwa hoja ya kutokuchukua hatua kwa NEMA bado ina utata wa kisheria.
Hatimaye, mahakama ilikubaliana na rufaa ya makanisa na kubatilisha uamuzi wa NET kwa ukamilifu.
Uamuzi huu umeondoa ulinzi uliokuwa umetolewa kwa hoteli hizo, na migogoro kama hiyo sasa italazimika kushughulikiwa kwa mifumo mingine ya kisheria.