PAWA!: Ruto aanza kujikuna kichwa kuhusu mustakabali wa baadhi ya wandani wake 2027 ikikaribia
RAIS William Ruto ameanza kujikuna kichwa kuhusu mustakabali wa baadhi ya wandani wake wa kisiasa, ODM ikisisitiza kuwa inanyemelea wadhifa wa naibu wa rais.
Wiki jana katika Kongamano la Wajumbe wa ODM, chama hicho kinachoongozwa na Dkt Oburu Oginga kilisisitiza kuwa lazima kiwe na maelewano ya kina na UDA kuzuia ‘kufanyiwa mchezo’ iwapo pande zote mbili zitafanikiwa kuupata uongozi wa nchi mwaka ujao.
Naibu Rais Prof Kithure Kindiki, Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavadi, Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula na mwenzake wa Seneti Amason Kingi ni kati ya wanasiasa ambao huenda ‘wakatolewa kafara’ kwenye nyadhifa zao katika makubaliano kati ya ODM na UDA.
Hata hivyo, baadhi ya wachanganuzi wa kisiasa wanasema kuwa kuachia ODM nyadhifa muhimu huenda kutamgharimu kisiasa Rais Ruto na kutikisa ngome yake.
Badala yake, wanasema Rais anastahili kuzingatia zaidi kufanikisha miradi ya mabilioni hasa ya miundomsingi katika ngome za ODM ili kupata uungwaji mkono wa kuridhisha.
ODM sasa inang’ang’ania unaibu rais, uongozi ndani ya bunge na wizara za hadhi kama Usalama wa Ndani, Fedha na Afya wanaposukuma makubaliano kati yao na UDA.
Dkt Oginga hivi majuzi alisisitiza kuwa macho yao yako katika wadhifa wa unaibu rais ambao unashikiliwa na Prof Kindiki.
“Baadhi ya watu walifasiri kauli yangu vibaya kwamba hatulengi unaibu rais. Hicho ndicho kiti tunacholenga kabisa,” akasema Dkt Oginga akiwa Mombasa, kauli ambayo ilionyesha wazi wanalenga wadhifa wa Prof Kindiki.
Naibu wa Rais ameanza kunyooka moyo akionekana kusalimu amri kusalia na wadhifa wake akisema nafasi za kisiasa si za kushikiliwa milele.
“Nafasi zote ni za muda, mimi ni kiongozi na kuna leo na hapo kesho,” akasema Prof Kindiki wiki jana akiwa Meru.
Kuhusu Bw Gachagua, Naibu wa Rais alisema hatajibizana naye tena na amemsamehe.
“Kama mzee wa Njuri Ncheke siwezi kubishana na ndugu yangu, nimemsamehe,” akasema.
Wandani wa Prof Kindiki nao wamechemkia ODM kutaka kiti cha unaibu rais, msimamo wao ukimweka Rais Ruto katika njiapanda zaidi.
Kiongozi wa Wachache, Junet Mohamed ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa ODM naye alisisitiza kuwa hawataachilia chochote wanachohisi kitawanufaisha katika uhusiano wao na UDA.
“Kila mahali ambapo tuna mbunge, gavana, seneta, mwakilishi wa kike na diwani lazima tuachiwe. Idadi yetu ndiyo nguvu yetu,” akasema Bw Mohamed.
“Tumewasikia baadhi ya watu wakiongea sana lakini ukicheza nasi basi pia tutawasilisha mwaniaji wa urais. Usitishe ODM kwa sababu nasi tunajua ngome zetu na washirika wetu wanajua ngome zao, kwa hivyo tuheshimiane,” akaongeza.
Iwapo shinikizo za ODM za kutaka wadhifa wa Prof Kindiki zitakosa kutimia basi watanyemelea kiti cha Bw Wetang’ula.
Masaibu ya spika huyo yanazidishwa na kukataa kwake kuvunja chama chake Ford Kenya ili kijiunge na UDA.
Pia Bw Wetang’ula amekosolewa kwa kutoa maamuzi yanayoegemea mrengo wa serikali na hata aliwahi kushutumiwa na marehemu Kiongozi wa ODM, Raila Odinga kwa hilo.
“Kukataa kuvunja Ford Kenya wakati ambapo Rais anaviunganisha vyama vyote ndani ya UDA ili kuwa na wabunge wengi huenda kutamponza kisiasa,” duru kutoka serikali zikaarifu.
Bw Mudavadi naye anashikilia wadhifa ambao haupo kwenye katiba na alishakata kauli kuwa ANC imejiunga na UDA hata kama mchakato huo uliharamishwa na mahakama.
Kwa sasa Bw Mudavadi anaonekana hana nguvu kisiasa ikizingatiwa hata waliokuwa wakishikilia nyadhifa ndani ya ANC wamepewa nafasi za chini za uongozi ndani ya UDA.
Wadhifa wa Spika wa Seneti Amason Kingi nao pia utamulikwa, Rais Ruto anapolenga kuridhisha ODM ili apate uungwaji mkono wake 2027.
Bw Kingi tayari ametangaza kuwa PAA haitakuwa na wagombeaji uchaguzini 2027 na watawaunga wale wa UDA japo chama hicho hakitavunjwa.
Wandani wa Rais wanaoshikilia wizara za Usalama wa Ndani, Afya, Ulinzi na Wizara ya Masuala ya Nje nao pia wameingiwa na baridi nafasi zao zitaenda na ODM.
Mawaziri Kipchumba Murkomen (usalama wa ndani), Aden Duale (afya), Soipan Tuya (Ulinzi) na Bw Mudavadi (masuala ya kigeni) watalazimika kutafutiwe wizara nyingine iwapo ODM itatengewa wizara hizo pamoja na ile ya fedha ambazo wanadai.